Makamu wa Rais, Dk
Mohammed Gharib Bilal jana aliwaongoza mamia ya wakazi wa Jiji la Dar es
Salaam, kuzika miili ya watu sita wa familia moja waliokufa katika ajali ya
moto wakiwa nyumbani kwao Kipunguni, Manispaa ya Ilala usiku wa kuamkia
Jumamosi iliyopita.
Katika maziko hayo
yaliyofanyika makaburi ya Airwing yaliyopo Ukonga Banana, ibada ya maziko
iliongozwa na Askofu Msaidizi wa Kanisa Katoliki, Jimbo Kuu la Dar es Salaam,
Eusebius Nzigirwa akisaidiwa na mapadri watano.
Umati wa wananchi ulianza
kufurika mapema, ingawa shughuli ya kuihifadhi miili ya marehemu hao ilianza
saa 7:08, baada ya kuwasili kwa Makamu wa Rais na kuendelea kwa saa sita
mfululizo hadi takribani saa moja usiku.
Makaburini hapo, majeneza
sita yalipangwa kila moja karibu na kaburi, huku baba wa familia, David Mpira
akitangulia kuzikwa kwa kutanguliza kiungo cha mguu wake kilichotambuliwa jana
asubuhi chumbani kwake na baadaye kuwekwa jeneza na kuzikwa rasmi.
Mpira, aliyekuwa askari
mstaafu wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), hadi mauti yanamfika alikuwa
Katibu wa kikundi cha wanamaombi wa kanisa hilo.
Baadaye alizikwa mke wa
Mpira, Celina Yegela (50) aliyekuwa mstaafu wa Shirika la Usafirishaji Mizigo
kwa Njia ya Ndege (DAHACO). Wengine waliokufa katika ajali hiyo na kuzikwa jana
ni Samuel Yegela aliyekuwa anajiuguza nyumbani kwa dada yake, Lucas Mpira mtoto
wa familia hiyo na wajukuu wake, Celina na Paulina Emmanuel.
Ndugu wa marehemu,
wakiongozwa na mtoto pekee wa familia hiyo aliyenusurika, Emmanuel Mpira, baba
wa watoto wawili waliokufa ambaye amepoteza pia wazazi wawili, mjomba na kaka
yake, waliangua vilio vya mara kwa mara huku baadhi yao wakipoteza fahamu.
Awali, mara baada ya
kuwasili kwa miili yao, Makamu wa Rais aliongoza kutoa heshima kwa marehemu hao
kwa kuangalia picha zao, akifuatiwa na Askofu Nzigirwa, Mawaziri Profesa Mark
Mwandosya na Dk Harrison Mwakyembe, Naibu Waziri Dk Milton Makongoro Mahanga,
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Mecky Sadiki, wanafamilia na baadaye
waumini wachache waliowakilisha umati wa wananchi waliohudhuria.
Katika ibada hiyo, Askofu
Nzigirwa alitoa salamu kutoka Jimbo Kuu la Dar es Salaam na kusema msiba huo
ulikuwa mzito, kutokana na kuondoa familia yote kwa wakati mmoja, huku akisema
majibu ya maswali waliyonayo watu wengi yapo kwa Mungu.
“Tumesikia kuwa vifo hivi
vimetokana na ajali, hivyo tunajiuliza kwa nini wasingeacha kuangalia
televisheni wasingekufa au vikosi vya ukoaji wangewahi wasingekufa, ni vyema
kuacha kujiuliza kwa nini, bali tumuombe Yesu awapokee katika ufalme wake,”
alisema.
Alisisitiza kuwa, familia
hiyo ilikuwa ikiishi kwa kumtumainia Mungu na kwamba hata kama walikuwa na
mapungufu yao, lakini hawakumwacha Mungu, hivyo tukio hilo la kuchukua familia
na watu wa rika tofauti, linafundisha jamii kuishi kwa kumtumikia Mungu.
Makamu wa Rais, akizungumza katika maziko hayo, alisema msiba huo ni mkubwa na aliwapa pole wafiwa na kuwaomba kuwa na moyo wa subira huku akiwaombea marehemu miili yao ilale mahali pema peponi.
Makamu wa Rais, akizungumza katika maziko hayo, alisema msiba huo ni mkubwa na aliwapa pole wafiwa na kuwaomba kuwa na moyo wa subira huku akiwaombea marehemu miili yao ilale mahali pema peponi.
Aliwasihi Watanzania
kujitahidi katika nyumba zao kuwa na vizimia moto na kuhakikisha
wanajitahidi kuweka madirisha au milango ya dharura kwenye nyumba
zao.
Aliwataka wakati wa
matukio ya moto, kuhakikisha wanapiga namba ya zimamoto 114 badala ya kupiga
namba za polisi.
No comments:
Post a Comment