Wahadhiri 398 wamesomeshwa na serikali ndani ya miaka
mitano ikiwa ni mkakati wa kuongeza wanataaluma hao ili idadi iendane na
ongezeko la vyuo na wanafunzi.
Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufunzi, Dk Shukuru
Kawambwa alitoa taarifa hiyo mwishoni mwa wiki katika Chuo Kikuu Kishiriki cha
Elimu Mkwawa (Muce) alipokuwa akielezea utekelezaji wa Mradi wa Sayansi,
Teknolojia na Elimu ya Juu (STHEP).
Alisema wahadhiri hao wamesoma katika vyuo mbalimbali nchini na nje
ya nchi chini ya utekelezaji wa mradi
huo. Kati yao, 188 walidahiliwa
katika Shahada ya Uzamivu na 208 ni wa Shahada za Uzamili.
“Kwa wale waliodahiliwa katika Shahada ya
Uzamivu, watumishi 57 ambao ni asilimia 30 ni wanawake na wale wa Shahada ya
Uzamili wanawake ni asilimia 21 (watumishi 44),” alisema.
Aliongeza kwamba, wanataaluma 203 walikuwa
wamehitimu mafunzo yao na 195 wakiwa katika hatua za mwisho.
Kawambwa alisema mradi huo pia umegharimia
ujenzi wa majengo mapya 25, ikiwa ni pamoja na kuyafanyia ukarabati
yaliyokuwepo katika vyuo vikuu saba vilivyo katika mradi huo ambayo yatatumiwa
na wanafunzi 47,622 nchini kote.
Majengo hayo pia yana jumla ya vyumba vya
ofisi 1,794 kwa ajili ya wahadhiri, wakufunzi, wakutubi, wataalamu wa maabara
na wengine.
Akizungumzia mipango ya baadaye baada ya
kumalizika kwa awamu ya kwanza ya STHEP, Kawambwa alisema wizara yake imeanza
kutekeleza mradi mpya kwa mkopo nafuu wa Benki ya Dunia ambao utadumu kwa miezi
18.
Alisema mradi huo utatumika kukamilisha miundombinu
na majengo yaliyokumbwa na ukosefu wa fedha katika mradi wa kwanza yakiwamo
majengo ya kufundishia yaliyokosa samani, umeme na pia uunganishwaji wa taasisi
nane kwenye mkongo wa taifa.
Waziri Kawambwa alisema mradi huo pia
utasaidia kufanya tafiti kuhusu mahitaji ya utaalamu na maarifa nchini na
kuandaa mradi wa STHEP awamu ya pili.
No comments:
Post a Comment