WAGONJWA WA SARATANI WAONGEZEKA BUGANDO


Idadi ya wagonjwa wa saratani katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando jijini, Mwanza imeongezeka kutoka 3,400 mwaka 2009 hadi  kufikia wagonjwa 10,200 mwaka jana.

Hayo yalibainishwa na Mkuu wa Idara ya Saratani, Dk Nestory Masalu wakati akitoa taarifa  juu ya hali ya maendeleo ya ugonjwa huo katika hospitali hiyo.
Alisema ongezeko hilo linachangiwa na huduma za uchunguzi nje ya kituo, uchunguzi wa awali ndani ya kituo, elimu na mazingira ambayo ni pamoja na Ziwa Victoria, shughuli za migodi na virusi vya Ukimwi.
Alisema kati ya asilimia 70 na  80  ya wagonjwa wa saratani wanaofika hospitalini hapo kwa ajili ya matibabu  huwa katika hatua ya mwisho ya ugonjwa ambayo husababisha matokeo ya matibabu yake yasiwe mazuri.
Dk Masalu alisema asilimia 30 ya watu wazima na asilimia 50 ya watoto hupona baada ya kukamilisha matibabu, lakini wengi wao huhitaji tiba shufaa.
Alisema wagonjwa 400 wamenufaika na huduma ya kipimo  ambacho huwawezea kujua saratani imefikia wapi, kwa kiwango gani tangu mwaka 2011 kilipoanza kufanya kazi.
Dk Masalu  alisema kwa ushirikiano wa Wataliano waliweza kufanya huduma nje ya hospitali katika kuchunguza saratani ya matiti na shingo ya kizazi ambapo akina mama 4,000 wamechunguzwa kwenye vituo mbalimbali.
Alisema kwa sasa Tanzania imekuwa ikiwaona wagonjwa 600,000 ambapo idadi hiyo itaongezeka ifikapo mwaka 2030 ambapo wagonjwa zaidi ya 800,000 wapya watapatikana.
Awali Mkurugenzi Mkuu wa BMC, Profesa  Kien Mteta alisema saratani ni ugonjwa wa vinasaba katika mwili wa binadamu ambapo hukosea kutengeneza seli za binadamu.

No comments: