Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar kimesema
hakitaunda tena Serikali ya Umoja wa Kitaifa baada ya kumalizika kwa uchaguzi
mkuu wa mwaka huu, kutokana na baadhi ya
washiriki wake kuvuruga utaratibu na misingi ya kuanzishwa kwa serikali hiyo.
Kauli hiyo imetolewa na Katibu wa Kamati
Maalumu ya Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM Itikadi na Uenezi Zanzibar,
Waride Bakari Jabu wakati alipozungumza
na waandishi wa habari katika Ofisi Kuu
ya CCM Kisiwandui mjini hapa Zanzibar.
Waride alisema makubaliano yanayotokana na
kuwepo kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa kwa sasa yameanza kuvurugwa na kukiukwa
kidogo kidogo katika misingi yake mikuu huku kauli za chuki na uhasama
zikitawala.
Alikumbusha viongozi wa vyama vya siasa kwamba
sababu za kuwapo kwa Serikali ya Umoja
wa Kitaifa ni tofauti za kisiasa na kauli za chuki ambazo zilisababisha kuwepo kwa malumbano ya
kisiasa katika majukwaa ya kisiasa.
Alisema kwa bahati mbaya, misingi hiyo sasa
imeanza kuyumba na kuporomoka kidogo huku matusi na kejeli kwa viongozi wakuu
wa serikali akiwemo Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein, zikichukua nafasi
kubwa.
“Chama Cha Mapinduzi kimesikitishwa sana na
kauli za chuki na uhasama, zinazotolewa na
Makamo wa Kwanza wa Rais Maalim
Seif Sharif Hamad ambazo zinaashiria
kuyumba kwa serikali ya umoja wa kitaifa na kurudisha chuki na uhasama,”
alisema.
Waride alifafanua kwamba CCM ambayo ni mshirika anayeunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa, inatamka bayana
kwamba haipo tayari kushiriki kuunda serikali hiyo baada ya uchaguzi mkuu wa
mwaka huu.
Alifahamisha CCM haikuwa na sababu ya kuunda
Serikali ya Umoja wa Kitaifa kwa sababu ilipata ushindi wa kutosha, uliowafanya
kuunda serikali. Hata hivyo ilifanya hivyo kwa ajili ya kukidhi matakwa ya
sheria.
“CCM haioni sababu tena ya kuwepo kwa serikali
ya umoja wa kitaifa kwa sababu wenzetu CUF wamekuwa wakitoa kauli za chuki na
uhasama zinazorudisha nyuma matarajio ya wananchi wa kuwepo maridhiano ya
kisiasa,” alisema.
Serikali ya Umoja wa Kitaifa iliundwa kisheria
mwaka 2010 baada ya vyama vikuu vya siasa visiwani hapa, CCM na CUF,
kujadiliana na hatimaye kufikia mwafaka wa kugawana madaraka, kuondoa siasa za
chuki, zilizotokana na machafuko ya mwaka 2005 wakati wananchi walipokuwa
wakipinga matokeo ya Uchaguzi Mkuu wa Rais.
Katika hatua nyingine, Kamati Kuu ya CCM
itakutana Jumamosi ijayo kujadili mambo mbalimbali.
Taarifa
iliyotolewa kwa vyombo vya habari, ilieleza kuwa vikao vingine muhimu vya chama
hicho, vinaendelea kufanyika kwa ajili ya kikao hicho cha juu.
No comments:
Post a Comment