Wahitimu sita wa mafunzo ya Jeshi la Kujenga
Taifa (JKT), wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu,
Dar es Salaam wakikabiliwa na mashitaka ya kufanya mkusanyiko usio halali.
Washitakiwa hao ni Mwenyekiti wa Umoja wa
wahitimu hao George Mgoba, Makamu Mwenyekiti Parali Kiwango, Katibu Linus
Steven na wahitimu wengine Emmanuel Mwasyembe, Ridhiwani Ngowi na Jacob
Mang’wita.
Wote walikana mashitaka na kurudishwa rumande kwa kuwa Mkurugenzi wa
Mashitaka (DPP) amewasilisha hati ya kuzuia dhamana dhidi yao.
Walifikishwa mahakamani hapo asubuhi na
kupandishwa kizimbani saa 10 kasoro jioni, wakikabiliwa na mashitaka matatu ya
kula njama, kufanya mkusanyiko usio halali na kushawishi wenzao kutenda kosa la
jinai.
Wakili wa Serikali, Nassoro Katuga akisaidiwa na Tumaini Kweka,
Hellen Moshi, Janethroza Kitali na Inspekta Jackson Chidunda, alidai mbele ya Hakimu Mkazi, Frank Moshi kuwa Februari 15 mwaka huu katika
eneo la Msimbazi Centre, Ilala Dar es Salaam, washitakiwa walipanga njama za
kutenda kosa.
Alidai siku hiyo katika eneo hilo, walifanya
mkusanyiko usio halali kwa lengo la kuandamana kwenda kwa Rais kulazimisha
wapewe ajira katika utumishi wa umma, jambo ambalo ni kinyume cha sheria na
lingesababisha uvunjifu wa amani.
Katika mashitaka yanayomkabili Mgoba, Kiwango
na Steven, wanadaiwa siku hiyo katika eneo hilo, walishawishi wahitimu wenzao
wa mafunzo ya JKT, kufanya maandamano kwenda kwa Rais kulazimisha wapewe ajira
katika utumishi wa umma jambo ambalo ni kinyume cha sheria.
Walikana
mashitaka yanayowakabili na upande wa Jamhuri ulidai upelelezi
haujakamilika. DPP amewasilisha hati ya kuzuia dhamana dhidi ya washitakiwa
hao, chini ya kifungu cha 148 (4) cha Mwenendo wa Makosa ya Jinai (CPA).
Hakimu Moshi alisema washitakiwa watarudi
rumande hadi Machi 6 kesi itakapotajwa kwa kuwa DPP amefunga dhamana yao kwa
muda mpaka atakapoona inafaa, hivyo Mahakama haiwezi kutoa masharti ya dhamana.
Awali, Makamu Mwenyekiti wa vijana waliohitimu
mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Parali Kiwango (25) mkazi wa Temeke
Mikoroshini alijisalimisha Makao Makuu ya Polisi, kwa Mkuu wa Kitengo cha
Upelelezi.
Amri ya kumtaka kiongozi huyo kujisalimisha
ilitolewa juzi na Kamanda wa Polisi, Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman
Kova.
No comments:
Post a Comment