Ndegevita ya Jeshi la Ulinzi la
Wananchi wa Tanzania (JWTZ), iliyokuwa
katika mazoezi, imeanguka na kuteketea moto huku rubani wake akiumia wakati
akijiokoa katika Uwanja wa Ndege wa Mwanza.
Taarifa hiyo ilitolewa Dar es
Salaam jana na Kurugenzi ya Habari na Uhusiano ya jeshi hilo. Ilieleza kuwa
ndege hiyo iliwaka moto baada ya ndege (mnyama) kuingia ndani ya injini moja
wakati ndege ikiruka.
Naibu Mkurugenzi wa kurugenzi
hiyo, Meja Joseph Masanja akizungumza na waandishi wa habari Makao Makuu ya
Jeshi hilo aliwataka wananchi wasipate hofu ndege hiyo imeungua moto katika
ajali ya kawaida.
Alisema ajali hiyo ilitokea jana
mchana katika uwanja wa ndege wa kijeshi wa Mwanza wakati ndegevita za jeshi
hilo zikifanya mazoezi ya kuruka.
Alisema ndege hiyo ya vita
ilikuwa ikiendeshwa na rubani Meja Peter Lyamunda ambaye alipoona ndege yake
ikiwaka moto aliruka kwa kutumia vifaa maalum hivyo hakupata majeraha makubwa
zaidi ya kuumia mguu.
Meja Masanja alisema kwa sasa
rubani huyo anaendelea vizuri na kwamba eneo ambalo ndege iliangukia hakukuwa
na madhara yoyote.
"Tumetoa taarifa hii kama
Jeshi ili wananchi wapate taarifa sahihi, wasipotoshwe ndege hiyo imeanguka na
kuungua moto baada ya ndege mnyama kuingia ndani ya injini moja," alisema
Meja Masanja.
Alisema wananchi waendelee na
shughuli zao kama kawaida ndege hiyo ilikuwa katika mazoezi ya kawaida pamoja
na ndege nyingine.
No comments:
Post a Comment