Mwakilishi wa Jimbo la
Magomeni kwa tiketi ya (CCM), Salmin Awadh Salmin (57) amefariki ghafla akiwa
katika eneo la Ofisi Kuu ya CCM Kisiwandui ambapo alikuwa katika shughuli zake
za kawaida za kichama.
Kwa mujibu wa taarifa za baadhi ya wajumbe waliohudhuria kikao hicho,
alikuwa akizungumza na baadhi ya wajumbe wenzake wa Baraza la Wawakilishi ndipo
ghafla alianguka na kufa papo hapo.
“Sisi tunamaliza kikao cha Sekretarieti tunapewa taarifa kwamba
ameanguka na ndipo alipofikishwa haraka katika Hospitali ya Mnazi Mmoja na
kufariki'alisema Khadija Hassan Aboud, Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM ambaye
alikuwa pamoja na Salmin.
Wakati huohuo, Jakaya Kikwete amempelekea Rais wa Zanzibar, Dk Ali
Mohamed Shein, salamu za rambirambi kuomboleza kifo cha mbunge huyo.
Salmin alikuwa pia Katibu wa Kamati ya Wabunge wa Chama Cha Mapinduzi
(CCM) katika Baraza la Wawakilishi.
Katika salamu zake, Rais Kikwete alisema: “Nimepokea kwa mshtuko na
masikitiko makubwa taarifa za kifo cha ghafla cha Mheshimiwa Salmin Awadh
Salmin, Mwakilishi wa Jimbo la Magomeni katika Baraza la Wawakilishi na
Mwenyekiti wa Kamati ya Fedha ya Baraza hilo ambaye nimejulishwa ameanguka
ghafla wakati akihudhuria kikao mjini Zanzibar.”
“Nakutumia Mheshimiwa Rais salamu za rambirambi za dhati ya moyo wangu
kuomboleza kifo hiki kikubwa. Aidha kupitia kwako, nawatumia salamu za
rambirambi wananchi wa Magomeni ambao wamepoteza Mwakilishi wao na Wajumbe wa
Baraza la Wawakilishi waliopoteza mwenzao na kiongozi wao.”
Ameongeza Rais Kikwete: “Kupitia kwako,vile vile, natuma pole nyingi
sana kwa familia, ndugu na jamaa wa Mheshimiwa Salmin kwa kuondokewa na mhimili
mkuu wa familia na mlezi. Wajulishe niko nao katika msiba huu mkubwa na kuwa
msiba wao ni msiba wangu pia. Napenda pia uwajulishe kuwa naungana nao katika
kumwomba Mwenyezi Mungu aiweke pema roho ya marehemu.”
No comments:
Post a Comment