Watu wawili wamekufa
papo hapo huku wengine 45 wakijeruhiwa baada ya basi la abiria
lililokuwa likitokea Dar es Salaam kwenda Mwanza kugongana uso kwa
uso na lori katika kijiji cha Vikonje wilayani Chamwino mkoani
hapa.
Kamanda wa Polisi Mkoa
wa Dodoma, David Misime, alisema kuwa ajali hiyo ilitokea saa
7.05 mchana wakati basi la Kidia lenye namba za usajili T663
AXL kugonga lori lenye namba za usajili T 496 CFG na trela lenye namba
za usajili T576 AZX Scania.
Alisema basi hilo
lilikuwa likitokea Dar es Salaam kwenda
Mwanza wakati lori lilikuwa
likitokea Dodoma kwenda Dar es Salaam.
Aliwataja waliokufa
katika ajali hiyo kuwa ni dereva wa lori, Fadhili Said (36) na
utingo wa basi, Chogo Chigunda.
Kamanda Misime alisema
ajali hilo ilitokea wakati dereva wa basi la Kidia, Adam Robert (34)
alipokuwa akilifuata gari lililokuwa likilipita gari la mbele yake.
Alisema dereva wa basi
baada ya kushindwa kulipita gari lililo mbele yake alikutana na lori lililokuwa
likija mbele yake na kusababisha ajali hiyo.
Alisema Jeshi la Polisi
wanamfuatilia dereva wa basi ambaye anatibiwa majeraha katika moja ya
hospitali mjini hapa.
Pia alisema majeruhi hao
bado walikuwa wakitibiwa katika Hospitali ya Mkoa wa Dodoma na
wengine wameruhusiwa kurejea nyumbani.
No comments:
Post a Comment