Takribani
miaka 15 imepita tangu ilipotokea ajali
katika kijiji cha Idweli wilayani Rungwe mkoa wa Mbeya, iliyosababisha
vifo vya watu walioungua wakichota petroli
kwenye gari lililopinduka.
Hata
hivyo, tukio la namna hiyo limejirudia tena kijijini hapo na safari hii watu
wawili, wamekufa na wengine 18 kujeruhiwa wakati wakichota mafuta kwenye gari lililopinduka.
Lori
hilo lilikuwa likisafirisha mafuta kutoka Dar es Salaam kwenda Malawi.
Lilipinduka kijijini hapo juzi.
Vifo
hivyo viwili vya wakazi wa kijiji hicho, Maria Pajela (18) na Wiliam Pascal
(38), vimetonesha makovu ya huzuni ya ndugu na jamaa wapatao 40 waliopoteza
maisha na kulazimu miili yao kuzikwa
kaburi moja, kutokana na kuharibika zaidi na kushindwa kutambuliwa.
Akitoa
taarifa juu ya ajali ya juzi saa 3
usiku, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mbeya, Ahmed Msangi (pichani) alisema waliofariki na
waliojeruhiwa, walikuwa katika harakati za kuiba mafuta kutoka katika gari aina
ya Scania lenye namba za usajili T 891
AQZ likiwa na tela lenye namba T 821 ARF.
Alisema
gari hilo mali ya Ailis Sanga, lilipakia petroli yenye ujazo wa lita 41,000,
likitoka Dar es Salaam kwenda Malawi.
Lilikuwa likiendeshwa na Zawadi Nyato (46) mkazi wa Sae jijini Mbeya akiwa na utingo wake, Frank
Yohana (24) mkazi wa Mbozi.
Baada
ya kufika kijijini hapo, liliacha njia na kupinduka. Dereva na utingo waliokolewa na kupelekwa kituo cha Polisi
Kiwira kupata fomu namba tatu ya kwa
ajili ya matibabu.
Kamanda
alisema baadhi ya wakazi, walivamia lori hilo na kutoboa tangi la mafuta, hali
iliyosababisha mafuta kuanza kumwagika na kusambaa maeneo mbalimbali ikiwemo
kwenye makazi ya watu.
Kwa
mujibu wa kamanda, watu hao hawakujali hatari iliyokuwa ikiwakaribia, badala
yake waliendelea kukinga mafuta kwa kutumia vyombo vyao zikiwemo ndoo, madishi,
karai na madumu.
“Wakati
wakiendelea na harakati za wizi huo,wakazi hao walijikuta wakiwa katika moto
mkubwa baada ya lori hilo kulipuka na hapo ndipo wawili kati yao wakapoteza
maisha na waliosalia kujeruhiwa vibaya,” alisema Kamanda.
Alitaja majeruhi katika ajali hiyo, ambapo wanaume ni 13 na wanawake watano ni
Shukuru Kanzale (21), Nuru George (30), Asante Boniface (38), Joseph Jamson
(18), Joseph Paschal (30), Siza Kanesa (22),Alex Daud (35), Oscar Yosia (23), Traiphon Moasi
(37) na Samson Mbwila (29).
Majeruhi
wengine ni Veronica Elia (30), Dora Michael(35), Rabsen Ayub (26), Wasiwasi Spika
(32), Asia Anon (20), Bahati Kyando (23),Christopher Erasto(32) na Melisa
Sanane (50) wote wakazi wa kijiji cha Idweli.
Kati ya majeruhi hao, 16 wamelazwa katika
Hospitali ya Misheni Igogwe na wawili wamelazwa Hospitali ya Serikali
Makandana, Tukuyu na hali zao zinaendelea vizuri.
Katika
tukio la mwaka 2000 katika kijiji hicho
cha Idweli, gari lililohusika lilikuwa likitoka Dar es Salaam kwenda
Malawi. Lilianguka kijijini hapo, kutokana na
utelezi katika mteremko unaoishia kwenye kijiji hicho.
Tukio
lingine la watu kuungua moto nchini, kutokana na kutaka kujipatia mafuta ya
bure, lilitokea mwaka jana katika eneo
la Mbagala Rangi Tatu, jijini Dar es Salaam la mwaka 2014.
Watu
wanne walipoteza maisha na wengine 21
kujeruhiwa vibaya baada ya kwenda kuchota mafuta yaliyokuwa yanamwagika wakiwa
na ndoo, vidumu vya lita tano na vyombo vingine bila kuchukua hadhari.
No comments:
Post a Comment