Mikoa sita
'imevurunda' katika ujenzi wa maabara katika shule za
sekondari baada ya kushindwa kufikia malengo. Ni mikoa mitatu pekee ndiyo
imefanya vizuri kwa kuvuka nusu ya malengo.
Waziri Mkuu,
Mizengo Pinda alitaja mikoa ambayo haikufika hata robo ya malengo kuwa ni
Mtwara (asilimia 21), Lindi (asilimia
20), Tabora (asilimia 17), Dodoma (asilimia 12), Rukwa (asilimia 11) na Kigoma
(asilimia 10).
“Tunaweza kusema
hii ndiyo mikoa ya mwisho katika kutekeleza agizo la Rais. Mikoa 16
ambayo sikuitaja hapa iko katika kundi la asilimia kati ya 26 hadi 49,” alisema
Pinda kupitia hotuba yake ya kuahirisha Bunge la 18.
Pinda alitaja
mikoa mitatu iliyofanya vizuri kuwa ni Njombe uliofanikiwa kukamilisha ujenzi
kwa asilimia 96 wa maabara za shule za sekondari, Ruvuma iliyokamilisha kwa
asilimia 81 na Morogoro ambao ni watatu kwa kujenga vyumba kwa asilimia 53.
Waziri Mkuu
alipongeza Ruvuma na Njombe kwa kutekeleza vizuri maelekezo ya Rais, akisema
imeonesha mfano mzuri. Alisema Morogoro ni wa tatu. Alisema Rais Jakaya
Kikwete katika hotuba yake kwa wananchi, Desemba 31 mwaka jana, aliongeza miezi
sita zaidi hadi Juni 2015 kwa ambao hawajakamilisha ujenzi wa maabara hizo, ili
wakamilishe.
Pinda alisema
matarajio ya Rais Kikwete ni kwamba muda huo unatosha kwa kila sekondari nchini
kuwa na vyumba vitatu vya maabara .
“Hivyo,
ninawataka wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya, mameya, wenyeviti na wakurugenzi
watendaji wa halmashauri za wilaya na miji nchini kuhakikisha maagizo haya
yanatekelezwa. Aidha, ninatoa rai kwa waheshimiwa wabunge na madiwani
kutoa msukumo stahiki katika utekelezaji wa maagizo haya kwa maslahi ya Taifa
letu,” alisema.
Kwa upande wa
Serikali, Pinda alisema Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za
Mitaa (Tamisemi), haina budi kuhakikisha agizo linatekelezwa ndani ya muda
uliotolewa; yaani Juni mwaka huu.
Aidha,
alisisitiza katika usimamizi, Tamisemi ihakikishe vyumba vya maabara
vinavyojengwa vinakuwa na ubora stahiki na vinalingana na thamani ya fedha
zilizotumika.
Amesema
ubadhirifu wa aina yoyote usipewe nafasi na watakaobainika kuhusika wachukuliwe
hatua za kisheria mapema.
“Nitapenda Ofisi
ya Waziri Mkuu, Tamisemi waendelee kufuatilia suala hili na kunipa taarifa mara
kwa mara,” alisema.
Mwaka 2012, Rais
Kikwete akiwa ziarani katika mkoa wa Singida, alielekeza kila shule ya
sekondari nchini iwe ina vyumba vitatu vya maabara ifikapo Novemba 30,
2014.
Tangu wakati huo
hadi sasa, utekelezaji unaendelea na kwa mujibu wa Waziri Mkuu, hali ya ujenzi
wa vyumba vya maabara inaonesha hadi Desemba mwaka jana, vyumba
3,607 sawa
na asilimia 34
ya mahitaji ya vyumba 10,653 vya maabara nchini vilikuwa vimejengwa.
Aidha, vyumba
6,249 sawa na asilimia 59 ya mahitaji, vilikuwa vinaendelea kujengwa na
asilimia saba vilikuwa havijaanza kujengwa.
Wakati huo huo
Pinda alisema bajeti ya uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapigakura ni Sh
bilioni 218 na ya Uchaguzi Mkuu Oktoba mwaka huu, ni Sh bilioni 268.
“Naelewa kwamba
changamoto kubwa ni upatikanaji wa fedha hizi kwa muda muafaka. Hata hivyo,
kipaumbele cha Serikali ni kuhakikisha kwamba fedha zinapatikana na kazi hii
muhimu inafanyika kama ilivyopangwa,” alisema.
Kuhusu Katiba
Inayopendekezwa, Waziri Mkuu alitoa mwito kwa wakuu wa mikoa wote nchini,
kuhakikisha wanasimamia kikamilifu usambazaji wa nakala zake.
Aidha ametaka
wananchi wahimizwe kusoma Katiba hiyo, ili washiriki kikamilifu katika upigaji
kura ya maoni utakaofanyika Aprili 30 mwaka huu.
No comments:
Post a Comment