TUME YA UTUMISHI WA WALIMU KUANZA KAZI JULAI


Serikali imesema Tume ya Utumishi wa Walimu itaanza kazi Julai  mwaka huu na kuhudumia walimu katika masuala mbalimbali huku muundo wa utumishi wa tume hiyo umehusisha ngazi za chini na juu.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Celina Kombani alisema serikali imekubali kuanzisha tume hiyo ya kuhudumia walimu nchini ili kuepuka walimu kuhudumiwa na wizara mbalimbali.
Alisema tume hiyo itaanza rasmi mwezi huo na kuingizwa kwenye bajeti ijayo, huku madeni ya walimu ya mishahara yakiwa ni  yaliyohakikiwa Sh bilioni sita na ambayo hayajahakikiwa ni Sh  bilioni tatu.
Alisema ili kukabiliana na madeni ya walimu, sasa serikali imeagiza taasisi zote ziweke kipaumbele katika malipo ya likizo iwe kulipwa mapema kama mishahara.
Awali, Kamati ya Huduma za Jamii ilitaka walimu nchini kusajiliwa ikiwa ni pamoja na wanaofanya kazi katika shule binafsi  ili kuwatambua walimu na kuweka kiwango cha msingi cha kutoa huduma kwa walimu nchini kwa kuitumia Tume ya Utumishi wa Walimu.
Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Margaret  Sitta alisema kamati inapongeza kusudio la serikali kuanzisha Tume ya Utumishi wa Walimu nchini katika mwaka wa fedha 2015/16.
Alisema kamati inashauri tume hiyo kuanzishwa haraka ili kukabiliana na adha zinazowakabili walimu nchini na kurejesha hadhi ya taaluma ya ualimu nchini. 

No comments: