HIZI NDIZO TAKWIMU ZA WATENDAJI WALIOADHIBIWA SERIKALINI

Wakurugenzi  21 katika Halmashauri mbalimbali nchini wamevuliwa madaraka katika kipindi cha mwaka 2013 hadi 2015 huku 27 wakipewa onyo na sasa kesi zao zikiwa mahakamani kwa tuhuma mbalimbali, ikiwemo matumizi mabaya ya fedha.

Aidha, wafanyakazi 233 wamefukuzwa kazi na mabaraza ya madiwani na wengine 372 kesi ziko mahakamani huku 10 zikiwa zimetolewa uamuzi wa kufungwa na wengine kutozwa faini.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi), Hawa Ghasia alisema hayo wakati akijibu hoja  za Kamati ya Kudumu ya Bunge  ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu madai ya kuhamisha watumishi wenye tuhuma bila kuwachukulia hatua.
Ghasia alisema iwapo kuna watumishi waliohamishwa bila kujua na inapofahamika wanarudishwa kituo cha kazi kujibu tuhuma kwani si sera ya wizara yake kuwahamisha kwa makusudi watumishi wanaotuhumiwa kwa makosa mbalimbali wanawachukulia hatua za kisheria.
Akizungumzia suala la miradi ya chini ya kiwango, alisema kuanzia mwaka jana wamepitia muundo wao na kuunda idara ya ufuatiliaji na tathmini ya ubora katika miradi ya halmashauri na ikiwa chini ya kiwango hatua zinachukuliwa kabla Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) hajafika kukagua.
Katika suala la kuongeza mapato katika halmashauri, alisema mwaka 2013 walifanya utafiti wa kuainisha vyanzo vipya vya mapato na kupata  ushuru wa minara ya simu, nyumba za kulala wageni na halmashauri kutoza kodi yamajengo.
“Lakini pia tunatarajia kurekebisha sheria  ya fedha katika serikali za mitaa na tayari rasimu ya kwanza  imekamilika kwa lengo la kuongeza vyanzo vya mapato katika halmashauri,” alisema.

No comments: