EWURA YAAGIZWA KUKOKOTOA UPYA BEI YA MAFUTA

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, imeitaka Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kufanya ukokotoaji upya wa bei ya mafuta ili kumsaidia mlaji wa mwisho wa bidhaa hiyo kunufaika na punguzo la bei ya mafuta duniani.

Akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa shughuli za kamati hiyo, Mbunge wa Tandahimba, Juma Njwayo (CCM) kwa niaba ya mwenyekiti wa kamati hiyo alisema utaratibu huo wa Ewura wa M-One wauangalie upya kwani unaumiza mlaji.
Alisema bei ya bidhaa hiyo duniani imeshuka kwa asilimia 60. Dar es Salaam hutumia asilimia 60 ya mafuta yanayoagizwa nchini huku kampuni zinazouza mafuta yanauza lita moja Sh 1,520 kwa jumla.
Njwayo alisema lakini katika vituo vya rejareja Dar es Salaam bidhaa hiyo huuzwa Sh 1,849 tofauti ya Sh 329 kwa lita moja, kwani  kutokana na kushuka kwa bei hiyo  ya mafuta duniani inaweza kushuka  kila mwezi.
Pia alisema kamati inashauri serikali kwa ushirikiano na wawekezaji binafsi kuanza ujenzi wa bomba la kusafirisha mafuta kutoka Dar es Salaam kwenda mikoani ili kupunguza gharama za mafuta, usalama wa usafirishaji pamoja na usalama wa barabara nchini.
Kamati hiyo iliishauri serikali kuachana na mitambo ya kukodi ya kampuni ya Songas-Gas, IPTL na Symbion kama ilivyofanya kwa Aggreko na kununua mitambo yake ili kuliondolewa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) gharama kubwa ya capacity charge kwani mitambo ya kukodi gharama yake ni kubwa.
Alisema Tanesco iweke mpango maalumu wa muda mfupi  kati na mrefu kukusanya madeni yote wanayodai watu binafsi, serikali na taasisi zake ambazo ni Sh bilioni 186.4 na kulipwa moja kwa moja kupitia hazina.
Akizungumzia suala la sekta ndogo ya gesi, alisema kamati imeridhishwa na hatua za kumalizia ujenzi wa bomba  gesi na miundombinu yote ifikapo Juni, mwaka huu.
“Hata hivyo, tunaomba serikali kuhakikisha Sera Mpya ya Gesi inawafikia wananchi na wadau wengi huku uagizaji mafuta kwa pamoja ukipunguza kero nyingi za upatikanaji wa mafuta na udhibiti wa bei ya bidhaa hiyo,” alisema Njwayo.
Aliitaka serikali kuandaa sera na sheria kuhusu masuala ya joto ardhi na mchakato huo kushirikisha wadau kwa lengo la kuwa na vyanzo mbadala vya umeme nafuu na endelevu nchini baada ya kuundwa kwa kampuni ya umma ya kusimamia tafiti, uanzishaji na uendelezaji wa miradi hiyo.

No comments: