SERIKALI YAONYWA KUHUSU UCHOKOZI WA JESHI LA POLISI


Wakati Jeshi la Polisi likilaumiwa kutokana na namna lilivyoshughulikia maandamano ya Chama cha Wananchi (CUF) wiki iliyopita, Serikali imetahadharishwa kuwa makini na harakati za kisiasa zinazotumia mbinu za kuchokoza Jeshi la Polisi na kuvunja sheria halali.

Wakizungumza na mwandishi wiki hii kuhusu dhana ya udhaifu wa jeshi hilo, baadhi ya watu wakiwemo wasomi wameitaka Serikali kuwa makini na kauli za wanasiasa, ambao wamewahi kushiriki au kutoa matamko ya kihalifu na leo wanatuhumu jeshi hilo.
Baadhi ya matukio ya kihalifu yaliyotajwa kufanywa katika mazingira ya siasa, tamko la maandamano na migomo isiyokoma, bila kibali cha Polisi, lililotolewa hivi karibuni na Mwenyekiti mwenza wa Ukawa, Freeman Mbowe na udhalilishwaji wa Mkuu wa Wilaya, wakati wa uchaguzi mdogo wa Igunga uliokuwa na ushindani wa kisiasa mwanzoni mwa 2011.
Tahadhari hiyo imetolewa, wakati Serikali ikielezea  kuridhishwa na kazi ya kutunza amani nchini inayofanywa na jeshi hilo, na kuagiza lijiandae na siasa za 2015; siasa za kabla ya Kura ya Maoni ya kupata Katiba Mpya na za kabla ya Uchaguzi Mkuu ujao.
Akitoa tamko kuhusu kudhibitiwa kwa maandamano ya CUF wiki iliyopita, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mathias Chikawe, akizungumzia hoja ya mwenyekiti mwenza wa Ukawa, James Mbatia (NCCR-Mageuzi), kuhusu polisi walivyodhibiti maandamano ya CUF,  alisema Profesa Ibrahimu Lipumba, ambaye pia ni Mwenyekiti mwenza wa Ukawa, alikaidi zuio la Jeshi la Polisi.
Akifafanua zaidi,  Chikawe alisema Januari 26 mwaka huu, Jeshi la Polisi lilipokea barua kutoka CUF, iliyokuwa ikitoa taarifa za kufanyika kwa maandamano kwenye viwanja vya Zakhiem Mbagala, Dar es Salaam.
“Maandamano yalipangwa kuanzia Temeke kwenda Zakhiem… Jeshi la Polisi liliwaita viongozi wa CUF kwa mazungumzo. Walifanya mazungumzo na Jeshi la Polisi lililotoa tahadhari kadhaa kutokana na sababu za kiusalama,” alisema Chikawe.
Pamoja na CUF kuonekana kama vile walielewa tahadhari hiyo, Chikawe alisema walishangazwa kuona Profesa Lipumba akikaidi zuio la Jeshi la Polisi na kuamrisha wananchi kuandamana kuelekea Zakhiem.
“Jeshi la polisi linataka kila mtu kutii sheria bila shuruti, na mtu yeyote akishindwa kufanya hivyo, Jeshi la Polisi litamshughulikia mtu bila kujali umri, jinsia, wala madaraka yake,” alieleza Chikawe kuonesha namna Lipumba alivyokaidi amri ya Polisi katika harakati hizo hizo za siasa za ushindani.
Akizungumza na mwandishi jana, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), katika masuala ya Utawala na Siasa, Dk Benson Bana, alishangaa Bunge kutumia fedha za umma, kujadili tukio la kiongozi mmoja katika jamii aliyevunja sheria.
“Tuna viongozi wengi kuanzia wa kiroho, wa kiutamaduni na wa kisiasa, inakuwaje kiongozi mmoja wa kisiasa akivunja sheria Bunge likae kujadili?” alihoji, akizungumzia mjadala wa Bunge kuhusu kukamatwa na kufikishwa mahakamani kwa Profesa Lipumba.
Aliwataka Watanzania kuwa macho na mbinu zinazotumika za kuchokoza vyombo vya dola na kukumbusha kuwa kuna chama kimoja, ambacho hakukitaja jina, lakini ni Chadema, kilichotoa tamko la kuhakikisha nchi haitawaliki mara baada ya kushindwa katika Uchaguzi Mkuu uliopita.
“Yapo matamko mengi tu, lipo hata la Mbowe la maandamano na migomo isiyokoma na katika matamko yote hayo, sijasikia siku hata moja vyama vya upinzani vikisema Jeshi la Polisi linafanya kazi vizuri.
“Kama unajua siasa za Tanzania, suala la kuchokozwa Polisi ni la kawaida lakini ni vyema vyombo vya habari vitusaidie, Polisi si chombo cha siasa ni cha amri, hakipaswi kuchokozwa… sisi tunalala usiku na kuamka salama dhamana ya usingizi wetu tunawapa wao,” alisema.
Akielezea namna wanasiasa wanavyopenda kuchokoza Polisi na vyombo vingine vya dola, alitoa mfano wa baadhi ya wanasiasa kusimamisha walinzi binafsi nyuma yao, wakati wakihutubia mikutano ya hadhara.
“Umeona katika nchi gani mwanasiasa anasimamisha mlinzi nyuma kama Rais, wanajifananisha na Rais? Hii ni hadaa, hawa wamelewa madaraka ambayo hawana,” alisema na kusisitiza umuhimu wa jamii kuelimishwa ili wanasiasa waache kupima nguvu na vyombo vya dola.
Moja ya matamko ya kuchokoza Polisi, ni lililowahi kutolewa na Mbowe la kufanya maandamano na migomo isiyokoma nchi nzima,  mwishoni mwa mwaka jana wakati wa Mkutano Mkuu wa Chadema.
Mbowe aliyekuwa akiomba kuchaguliwa katika nafasi hiyo kwa mara ya tatu mfululizo, na hivyo kuvunja utamaduni wa chama hicho wa tangu kilipoasisiwa, kwa  kiongozi kuongoza kwa muda usiozidi vipindi viwili vya miaka mitano, alitoa tangazo hilo kushinikiza kuvunjwa Bunge Maalumu la Katiba.
“Natangaza azimio la Mkutano Mkuu ni kushirikisha umma kwa maandamano na migomo kwa kibali cha polisi na bila kibali...siko tayari kwa mazungumzo tena, nchi haiwezi kubadilika kwa mazungumzo ambayo ni kuchezea fedha za umma.
“Najua watatumia nguvu na kututisha na silaha za moto. Lakini sisi tutasonga mbele,” alisema na kutaka kuundwe mtandao wa Chadema  na wananchi kushirikiana na Ukawa kila wilaya, kufanya maandamano na migomo hiyo.
Aidha, aliagiza wanasheria wote wa Ukawa wakutane na kuona uwezekano wa kufungua kesi dhidi ya wajumbe wa Bunge hilo, kuwashambulia kisiasa wajumbe ambao ni wabunge katika majimbo yao ili kuhakikisha hawarejei tena katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.
Wakati mbinu hiyo ya kisiasa ikijionesha hadharani, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mohammed Aboud Mohammed, amelitaka  Jeshi la Polisi nchini kujipanga kukabiliana na vurugu za kisiasa za 2015.
Mohammed Aboud, ambaye amewahi kuwa Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi wa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, amesema vurugu hizo zimeanza kuonekana wakati nchi ikielekea kwenye upigaji Kura ya Maoni ya Katiba Inayopendekezwa na Uchaguzi Mkuu.
Alisema hayo juzi jioni wakati akifunga mkutano wa maofisa wakuu waandamizi wa Jeshi la Polisi uliokuwa ukifanyika mjini Dodoma, na kuongeza kuwa Serikali imeridhika na utendaji wa Jeshi la Polisi katika kuimarisha amani na usalama katika nchi.
“Sasa si tu suala la uhalifu, harakati za kisiasa husababisha kupotea kwa hali ya usalama na kuleta vurugu… ni lazima kutengeneza mikakati ya kukabiliana na hali hiyo,” alisema.
Alifafanua kuwa mikakati itakayowekwa, inapaswa iwe kwa ajili ya kusaidia kufanikiwa kwa Kura ya Maoni na Uchaguzi Mkuu, ili shughuli hizo muhimu kwa mwaka huu, zifanyike kwa usalama na utulivu.
“Mjipange mapema na kujitayarisha na rasharasha zinazoonekana ili wakati utakapofika, mkabiliane na hali halisi na Serikali itafanya kila linalowezekana kulinda amani iliyopo,” alisema
Alisisitiza licha ya askari Polisi kufanya kazi katika mazingira magumu, lakini wamekuwa na bidii katika kuhakikisha Taifa linakuwa katika hali ya usalama na kuipa Tanzania sifa ya kuwa kisima cha amani.
Hata hivyo akizungumzia dhana ya udhaifu wa Jeshi hilo, Mohammed Aboud alisema katika Jeshi hilo kuna wakorofi wachache ambao kwa njia moja au nyingine wanalitia doa Jeshi hilo.
“Lazima viongozi wa Jeshi muwe na utaratibu wa kutengeneza njia ya kuwashughulikia wanaoharibu jina la jeshi ili waache tabia hiyo na wachukuliwe hatua kabla ya kuharibu,” alisema.
Alitaja baadhi ya mambo yanayolalamikiwa sana kuwa ni unyanyasaji wa vijana, kubambikia kesi, kutoa siri za raia, kuchelewesha upelelezi, kutofika kwa wakati kwenye tukio na vitendo vya rushwa.
Akizungumzia dhana hiyo ya udhaifu, Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini,  Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Ernest Mangu, alisema katika mkutano huo walifanya tathimini kuhusu maeneo waliyofanya vizuri na yale yasiyofanywa vizuri.
“Tumeona uwezo wetu kwenye utendaji, tumeandaa maazimio      yatakayoeleza namna nzuri ya kujipanga,” alisema.
Alisema sasa wanajipanga kuona hali ya usalama inaimarishwa wakati nchi ikielekea kwenye Kura ya Maoni na Uhaguzi Mkuu.
“Utendaji mzuri ni ule wenye weledi na unaozingatia haki za binadamu,” alisema.

No comments: