FEDHA ZAKWAMISHA KUKAMILIKA MRADI WA DART


Mradi wa Mabasi yaendayo Haraka Dar es Salaam (DART) unakabiliwa na changamoto ya kifedha katika ujenzi wa miundombinu,  kutokana na ongezeko la mahitaji ya fedha za kuukamilisha.  

Bunge lilielezwa kwamba ongezeko la mahitaji ya fedha za kukamilisha mradi huo ni Sh bilioni 64.7, ambazo kati yake Sh bilioni 20.6 ni ongezeko la mishahara na Sh bilioni 44.1 ni ongezeko la kazi na madai mengine.
Mjumbe wa Kamati ya Bunge ya Tawala za Mikoa  na Serikali za Mitaa, Dk Athuman Mfutakamba alisema hayo jana wakati akiwasilisha taarifa ya mwaka ya kamati kuanzia Januari 2014 hadi 2015.  
Kamati  hiyo imeishauri serikali kufanya jitihada za makusudi, kuhakikisha mradi unaendelea kutekelezwa kama ilivyopangwa na fedha yote inayohitajika kukamilisha hatua mbalimbali za mradi, zinatengwa na kupelekwa hatua zikamilike kwa wakati.  
Kwa mujibu wa Mfutakamba, inadaiwa ongezeko hilo limefanya mkandarasi kutoonesha utayari wa kuanza kazi katika barabara ya Msimbazi kwa hofu ya kutokuwepo kwa fedha za kumlipa.  
Changamoto nyingine ambayo wabunge walielezwa kwamba inakabili mradi, ni uharibifu wa miundombinu ambao baadhi ya wananchi na wafanyabiashara ndogo huvamia maeneo ya ujenzi yanayoendelea.
Vile vile kumekuwapo tabia ya wizi wa samani za barabara, mifuniko ya maji ya mvua, maji taka na huduma nyingine.

No comments: