KUPE WAKUBWA WATUMIKA KUKABILIANA NA UKEKETAJI


Wanawake  wa Kimasai wanaopinga suala la tohara kwa watoto wamegundua njia nyingine ya kukabiliana na ukeketaji kwa kutumia kupe wakubwa.

Hayo yalielezwa katika warsha ya kujipanga kupokea mradi wa kijiji cha dijitali, iliyofanyika katika kijiji cha Ololosokwan hivi karibuni.
Wakijadili changamoto ya ukeketaji kama sehemu ya shida kubwa ya jamii kiafya, wanawake wamesema kwamba hukamata kupe wakubwa na kuwaua kisha kupiga vigelegele kuonesha kwamba mabinti wao wamepewa tohara.
Mmoja wa washiriki wa warsha hiyo alipouliza inakuwaje  hapo baadaye binti anapokuwa mkubwa, aliambiwa kwamba ni rahisi kwa binti huyo hapo baadae kuzungumza na mwenzake wakaelewana.
“Tatizo la tohara ni la wanaume, wanaume hawa ndio wanahimiza wanawake wawe na tohara kwa kuwa wanataka kuwaoa wanawake ambao wameingia tohara kama wao,” alisema mama mmoja.
Alisema namna hiyo imefanya kuwakwepesha mabinti wengi na vurugu za tohara, ambazo kiafya si sawa, hasa kutokana na tatizo linaloambatana na kovu wakati wa uzazi na pia kwenye  uhusiano wa kimapenzi kwa upande wa mwanamke.
Katika warsha hiyo, ambapo pia suala la ndoa za utotoni na mimba za utotoni zilijadiliwa,  ilielezwa kuwa elimu inatakiwa kupewa watu wa mila ili kutambua athari za mimba na ndoa za utotoni.
Kijiji cha dijitali cha Ololosokwan, kinatarajiwa kuwa na huduma zote za kijiji cha kisasa kama umeme, afya na kituo cha utamaduni, ambacho kitaunganisha watalii na wananchi ili kuwawezesha kiuchumi.

No comments: