BEI YA MAFUTA YAZIDI KUPOROMOKA


Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), imetangaza kushuka zaidi kwa bei za bidhaa za mafuta hapa nchini kuanzia leo, kutokana na bei katika soko la dunia kuendelea kuporomoka.

Mwezi uliopita, kwa mara ya kwanza baada ya muda mrefu, bei ya petroli, dizeli na mafuta ya taa ilishuka kwa kiasi kikubwa, mathalani bei ikifikia chini ya Sh 2,000. Na jana, bei ya juu kabisa ya petroli ilitangazwa kushuka kwa Sh 187 zaidi.
Nafuu hiyo ya bei ilitangazwa na Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Felix Ngamlagosi, akisema bei hizo za kikomo za bidhaa ya mafuta zitaanza kutumika leo nchi nzima na kwamba mabadiliko hayo ya bei yanatoka na kushuka kwa bidhaa hiyo katika soko la dunia.
Alisema bei za jumla na rejareja kwa aina zote za mafuta yakiwemo petroli, dizeli na mafuta ya taa zimeshuka, ikilinganishwa na bei katika toleo lililopita la Januari 7, mwaka huu.
“Katika toleo hili bei za rejareja kwa petroli zimepungua kwa Sh 187 kwa lita sawa na asilimia 9.56, dizeli imepungua kwa Sh 139 kwa lita sawa na asilimia 7.53 na mafuta ya taa yamepungua kwa Sh 177 kwa lita sawa na asilimia 9.64,” alisema.
Aidha, alisema kwa kulinganisha matoleo hayo mawili bei za jumla zimepungua ambapo petroli imepungua kwa Sh 186.89 kwa lita sawa na asilimia 10.08, dizeli Sh 138.97 kwa lita sawa na asilimia 7.97 na mafuta ya taa kwa Sh 176.64 kwa lita sawa na asilimia 10.20.
“Bei za mafuta masafi katika soko la dunia kwa petroli, dizeli na mafuta ya taa zimepungua kati ya mwezi Julai na Desemba 2014 kwa takribani dola 440 kwa tani, dola 304 kwa tani na dola 324 kwa tani sawia sawa na punguzo la asilimia 44,35 na 35 sawia,” alisema.
Alisema kati ya mwezi Septemba 2014 na Februari 2015, bei za petroli, dizeli na mafuta ya taa katika soko la ndani zimepungua kwa Sh 499 kwa lita, Sh 384 kwa lita na Sh 384 kwa lita sawia, ambayo ni sawa na punguzo la asilimia 22, 18 na 19 sawia.
"Katika kipindi husika, thamani ya shilingi ya Tanzania ikilinganishwa na dola ya Marekani imeshuka kwa asilimia 6. Bei ya mafuta kwenye soko la ndani ingeweza kupungua zaidi kama thamani ya shilingi isingeendelea kudhoofu," alisema.
Pia, Ngamlagosi alisema ni muhimu kuzingatia kwamba kwa wastani bei za mafuta katika soko la dunia na gharama za uagizaji (CIF) huchangia asilimia 60 ya bei ya mafuta katika soko la ndani, hivyo kiwango cha ushukaji bei katika soko la ndani hakiwezi kuwa sambamba na asilimia ya ushukaji katika soko la dunia.
"Kampuni za mafuta zipo huru kuuza bidhaa za mafuta ya petroli kwa bei ya ushindani ilimradi bei hizo ziko chini ya bei ya kikomo kama ilivyokokotolewa na fomula iliyopitishwa na EWURA na ambayo ilichapwa kwenye gazeti la serikali namba 354 la Septemba 26, 2014," alisema.
Alisema vituo vyote vya mafuta vinatakiwa kuchapisha bei za bidhaa za mafuta katika mabango yanayoonekana bayana na yakionesha bei ya mafuta, punguzo, vivutio vya biashara au promosheni zinazotolewa na kituo husika.
"Pale ambapo inawezekana kuchagua wateja wanashauriwa kununua bidhaa za mafuta kutoka kwenye vituo vinavyouza mafuta kwa bei ndogo zaidi ili kuimarisha ushindani. Ni kosa kuuza mafuta bila kuweka mabango ya bei inayoonekana vizuri kwa wateja na adhabu itatolewa kwa kituo husika," alisema.
Aidha aliwataka wanunuzi kuhakikisha wanapata stakabadhi ya malipo inayoonesha jina la kituo, tarehe, aina ya mafuta yaliyonunuliwa na bei kwa lita.
Alisema stakabadhi hiyo ya malipo itatumika kama kidhibiti cha mnunuzi wa mafuta endapo kutajitokeza malalamiko ya ama kuuziwa mafuta kwa bei ya juu kuliko bei kikomo au endapo mnunuzi atakuwa ameuziwa mafuta yenye kiwango cha ubora kisichofaa.
Alisema bei za kikomo kwa Dar es Salaam bei za rejareja kwa lita moja ya petroli ni Sh 1,768,  dizeli Sh 1,708 kwa lita na mafuta ya taa ni Sh 1,657 kwa lita huku bei za jumla ikiwa ni Sh 1,666.43 kwa lita ya petroli, Sh 1,605.52 kwa lita ya dizeli na Sh 1,554.59 kwa lita ya mafuta ya taa.
Hata hivyo, alizitaka mamlaka mbalimbali kuhakikisha zinawawezesha wananchi kuona manufaa ya kupungua kwa bei ya bidhaa hiyo hasa katika sekta ya usafirishaji na nishati ya umeme.
Pamoja na nafuu hiyo ya bei, wataalamu mbalimbali wa masuala ya uchumi, wakiwemo wanasiasa waliohoji kwa muda mrefu sababu za kutoshuka kwa bei ya mafuta nchini, hawakuwa tayari kuzungumzia mapema juu ya punguzo hilo la bei.
Zitto Kabwe, Mchumi na Mbunge wa Kigoma Kaskazini anayeiongoza Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), alipotafutwa kuzungumzia hilo, alisema hajapata taarifa rasmi, hivyo hatakuwa tayari kusema lolote.
Hata hivyo, shauku ya Watanzania wengi ni kuona kwamba, gharama za maisha, zikiwemo za usafiri na usafirishaji zinazoumiza wengi kwa kile kinachodaiwa kupanda kwa gharama za vipuri na hata nishati ya mafuta.

No comments: