WANNE FAMILIA MOJA WAFA KWA CHAKULA CHENYE SUMU

Watu wanne wa familia moja wakazi wa kijiji cha Kibambila wilayani Kakonko mkoa wa Kigoma wamekufa na mtu mmoja amenusurika kifo kutokana na kula chakula kinachosadikiwa kuwa na sumu.

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo, Mganga wa zamu katika Kituo cha Afya cha Kakonko, Ndalikunda Kweka alisema kuwa watu hao walifikishwa kituoni hapo wakiwa na hali mbaya na baadaye wote wanne walifariki dunia wakati wahudumu wa afya wakijitahidi kuokoa maisha yao.
Mganga Mkuu wa wilaya ya Kakonko, Fadhili Seleman aliwataja watu waliokufa kuwa ni Neema Joseph (12), Jonas Joseph (18), Yusuph Joseph na Majaliwa Joseph (11).
Alisema kuwa uchunguzi wa awali uliofanywa na wahudumu wa afya kituoni hapo na baada ya kumhoji mtu aliyenusurika kwenye tukio hilo unaonesha kuwa watu hao walikula ugali unaosadikiwa kuwa ulikuwa na sumu.
Baba mzazi wa watoto waliokufa kwenye tukio hilo, Joseph Kajolo alisema kuwa aliweza kunusurika kuingia kwenye janga hilo kwa kuwa siku ya tukio hakula chakula hicho kwa kuwa alirejea nyumbani akiwa amelewa.
Mzazi huyo alisema kuwa hata hivyo pamoja na kunusurika huko hajui kama sumu hiyo ilikuwa kwenye unga uliotumika kupikia ugali huo au kuna mtu aliyeiweka baada ya ugali huo kupikwa.
Naye Mkuu wa wilaya ya Kakonko, Peter Kiroya alisema kuwa polisi wilayani humo inamshikilia mtu mmoja ambaye jina lake linahifadhiwa kwa sasa kutokana na sababu za kiusalama akituhumiwa kuhusika kuweka sumu kwenye chakula hicho.
Sambamba na kukamatwa kwa mtu huyo, Toyima ametoa wito kwa wakazi wa wilaya hiyo kuacha mchezo wa kuwekeana sumu kwenye vyakula na kusababisha mauaji kwani kwa sasa tabia hiyo imeanza kuota mizizi kwenye wilaya hiyo.

No comments: