TAZARA WALIPWA MISHAHARA YA MIEZI MINNE

Wafanyakazi wa Mamlaka ya Reli ya Tanzania na Zambia (TAZARA) waliokuwa wakidai mishahara yao ya miezi mitano, jana walilipwa sehemu ya madai hayo.
Wafanyakazi hao 1,500 waliokuwa wakiidai menejimenti ya mamlaka hiyo mishahara ya miezi mitano, wamelipwa mishahara ya miezi minne.
Akizungumza na mwandishi, Kaimu Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Reli Nchini (Trawu) Kanda ya Dar es Salaam, Yassin Mleke alithibitisha wafanyakazi kulipwa mishahara yao ya miezi minne badala ya mitano ambapo alisema, leo watakutana na kujadili mambo mbalimbali ikiwemo mishahara ya wafanyakazi iliyobaki.
Alisema licha ya kulipwa mishahara hiyo, maamuzi ya mwisho ya nini kitafanyika baada ya malipo hayo, yatatolewa katika mkutano wa pamoja kati ya TUCTA, TRAWU na wafanyakazi leo asubuhi.
Amesema hata hivyo hawatafanya mgomo kutokana na kuwepo kwa amri ya Mahakama Kuu.
Januari 15, mwaka huu Mahakama ilitoa amri ya kuwataka wafanyakazi hao kurudi kazini, huku ikiwaagiza kutofanya migomo isiyofuata sheria.
“Tumeingiziwa mishahara ya miezi minne, kwa hiyo kesho (leo) tutakutana na wafanyakazi wote na tutatoa maamuzi lakini siyo kufanya mgomo kwa sababu hatutaki kushindana na Mahakama yetu,” alisema Mleke.
Wafanyakazi hao waligoma kushinikizwa kulipwa mishahara yao ya miezi mitano na kutaka kukutana na Waziri wa Uchukuzi, Dk Harisson Mwakyembe ili kujadili hatma ya mamlaka hiyo pamoja na wafanyakazi wake.
Mgomo huo ulisababisha shida ya usafiri wa treni kwa abiria, hali iliyowalazimu menejimenti ya mamlaka kurudisha nauli kwa baadhi ya abiria waliokuwa wakitarajia kusafiri kwa treni hiyo.
Aidha, mbali na kuathiri safari za treni ya kwenda Bara, pia ilisababisha adha ya usafiri kwa abiria wa Jiji la Dar es Salaam, wanautumia treni ndogo ya kutoka stesheni ya Tazara hadi Pugu, Mwakanga.

No comments: