SERIKALI YAZIPIGA ‘STOP’ SHULE BINAFSI


Waziri  wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa amesema Serikali itazinyang'anya leseni ya uendeshaji shule binafsi, ambazo zimeweka viwango vyake vya ufaulu kwa wanafunzi wanaosoma kwenye shule hizo, tofauti na viwango vya Serikali.

Akijibu swali bungeni jana, Dk Kawambwa alisema iwapo shule hizo zitashindwa kufanyia kazi maelekezo ya wizara yake, hakutakuwa na njia nyingine, bali shule hizo kusitishiwa uendeshaji wake kwa kuzinyang'anya leseni.
Dk  Kawambwa alitumia fursa hiyo, kuonya shule binafsi kuhakikisha zinatekeleza maagizo ya Serikali ambayo yanazitaka kusitisha mfumo wake wa kuweka viwango vyao vya alama ya ufaulu wa mitihani.
Waziri huyo alikuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalumu,  Conchesta Rwamlaza (Chadema) ambaye alikuwa anataka kufahamu kama Serikali inafahamu kwamba shule binafsi zimeweka  viwango vyao wa alama za ufaulu.
Katika swali lake, Rwamlaza aliongeza kuwa wanafunzi ambao wanashindwa kupata alama zilizowekwa na shule binafsi, wanalazimishwa kukariri darasa au kufukuzwa shule.
Alisema hali hiyo imekuwa inawaathiri wazazi ambao wanapata mzigo wa kuendelea kulipa ada, lakini pia hali hiyo inawapotezea muda wanafunzi hao.
 “Hizi shule binafsi kwanza ada zake ziko juu; lakini pia zina mfumo wao nje ya mfumo wa Serikali ambao unawaathiri wanafunzi na wazazi. Wengi wa wanafunzi ambao wanashindwa kufikisha alama zilizowekwa na shule husika  wanalazimishwa kurudia darasa," alisema.
Aliongeza kuwa imefikia kiwango hata wanafunzi ambao wako kidato cha nne, ambao wanategemea kufanya mtihani wa kitaifa wanafukuzwa kwa sababu tu wameshindwa kufikisha ufaulu wa alama zilizowekwa na shule binafsi.
Kwa hali hiyo mbunge huyo, alitaka kufahamu hatua zinazochukuliwa na Serikali kuhakikisha mfumo huo unapigwa marufuku na Serikali.
Katika majibu yake, Dk Kawambwa aliwaelekeza maofisa elimu wa mikoa na wale wa wilaya, kuhakikisha shule zote za Serikali za binafsi zinatekeleza maagizo ya Serikali ambayo yametolewa na wizara hiyo inayosimamia utoaji wa elimu na sio vinginevyo.
 “Kuna maelekezo mengi ambayo tumeyatoa kwa shule zote likiwemo hili la alama za ufaulu na shule binafsi zinatambua hilo kwamba zikienda kinyume na agizo la wizara hatua inayofuata ni kufungwa kwa shule hizo," alisema Dk Kawambwa.
Alisema hakuna njia nyingine kwani serikali inataka kuhakikisha kwamba maelekezo yake yanatekelezwa.
Alitoa mwito kwa wananchi kutoa taarifa kwa shule ambayo inafanya mambo kinyume na maagizo hayo ya serikali ili hatua ziweze kuchukuliwa.

No comments: