Washitakiwa wa kesi ya mauaji ya Mjumbe
wa Tume ya Taifa ya Mabadiliko ya Katiba, Dk Edmund Mvungi (pichani), jana waligoma
kutoka katika chumba cha mahakama na kukaa kizimbani kwa muda hadi
watakapoelezwa jalada la kesi yao lipo wapi.
Tukio hilo ni la
jana asubuhi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu baada ya Wakili wa
Serikali, Peter Njike kudai kesi imekuja kwa ajili ya kutajwa, lakini jalada bado lipo kwa Mkurugenzi wa
Mashitaka (DPP).
Mshitakiwa, Longishu Losingo alidai “Desemba
12 mwaka huu upande wa Jamhuri ulidai jalada lipo kwa DPP na leo (jana) wanaleta hadithi, tunaomba
tuambiwe uhalali wa kesi hii kwa sababu tunateseka” .
Mshitakiwa mwingine, Masunga Makenza
alidai shitaka hilo ni la muda mrefu,
pia hawaifahamu sheria, lakini wanahitaji kujua DPP anaweza kukaa na
jalada kwa muda gani?
Wakili wa Serikali, Njike, alidai wamesikia malalamiko hayo,
ambayo yanatokana na kuchelewa kukamilika hivyo watafuatilia ili wakamilishe
upelelezi mapema. Alisema pia hakuna sheria inayomuongoza DPP kukaa na jalada
na kwa muda gani.
Hata hivyo, Longisho ambaye alikuwa
mlinzi wa nyumbani kwa Dk Mvungi, alidai wamechoka na hawana ugomvi na mahakama
wala magereza, lakini wana ugomvi na upande wa Jamhuri. Alidai kama Jamhuri imeshindwa kukamilisha upelelezi,
warudishwe polisi.
Aidha, Makenza alidai wapo tayari
kushitakiwa, lakini kama mashitaka hayo yangekuwa ya kweli, upelelezi ungekuwa
umekamilika. Alidai kama upande wa Jamhuri, haujakamilisha upelelezi wawaachie
halafu ukikamilika wakamatwe tena,
lakini siyo kudanganywa.
“Kwa hoja zilizotolewa na upande wa
Jamhuri leo hatupo tayari kushuka kizimbani hadi tutakapoelezwa jalada letu
lipo wapi na tunakaa chini,” alidai Makenza.
Baada ya kutoa kauli hiyo, washitakiwa
wote 10, isipokuwa mshitakiwa mmoja ambaye hakufika mahakamani hapo jana,
walikaa chini kwenye kizimba cha mahakama, wakisubiri waelezwe hatma ya jalada
la kesi yao.
Hakimu Mkazi, Hellen Riwa aliwasihi
wasifanye hivyo, bali wakubali kurudi mahabusu kwa kuwa kesi hiyo, imeletwa
kwake kwa ajili ya kutajwa na kupangiwa tarehe nyingine.
Aliwataka washitakiwa wawasilishe
malalamiko yao kwa Hakimu Mkazi, Waliarwande Lema anayesikiliza kesi hiyo. Washitakiwa walikubali kuondoka mahakamani
hapo huku wakisema Hakimu Lema akirudi watamlalamikia vikali.
Hii siyo mara ya kwanza kwa washitakiwa
hao, kufanya matukio mahakamani hapo, Desemba 6 mwaka jana waliiomba mahakama
iangalie uwezekamo wa kuwatenganisha gereza kwa sababu wakikaa pamoja
wanapigana, na wanaweza kuuana.
Mbali na Losingo na Makenza,
washitakiwa wengine ni Chibago Magozi (32), John Mayunga (56), Juma Kangungu
(29), Paulo Mdonondo (30), Mianda Mlewa (40) , Zacharia Msese (33) Msigwa
Matonya (30) na Ahmad Kitabu (30).
Wanadaiwa kuwa Novemba 3 mwaka jana katika eneo la
Msakuzi, Kibwegere, walimuua Dk Edmund Sengondo Mvungi kwa kukusudia.
No comments:
Post a Comment