Hivi ndivyo hali ilivyokuwa jijini Dar es Salaam baada ya mvua kubwa kunyesha kwa takribani saa mbili mfululizo. |
Mvua iliyonyesha jijini Dar es Salaam,
imeleta balaa baada ya kuua watu wawili, katika maeneo tofauti ya jiji,
likiwemo tukio la mtoto wa miaka minane kufa baada ya kuzidiwa na maji
yaliyoingia ndani ya nyumba aliyokuwa amelala.
Kwa mujibu wa taarifa ya Kamanda wa
Polisi Mkoa wa Kinondoni, Camillius Wambura, matukio hayo yalitokea mchana
kwenye maeneo mawili tofauti.
Tukio moja ni la Tandale, ambako mtoto Nasma Ramadhani (8), akiwa amelala
ndani ya nyumba yao, maji ya mvua iliyokuwa ikinyesha yaliingia ndani na
kumzidi nguvu kisha kusababisha umauti
wake.
Kamanda Wambura alisema mvua
iliyonyesha saa 5:00 asubuhi
ilinyesha kwa wingi, hivyo kuleta
madhara ya kujaa maji kwenye barabara kadhaa na pia kuleta maafa hayo ya vifo.
Katika tukio la pili, lililotokea
Mwananyamala, mvua hiyo ilisababisha kifo cha ajuza, Habiba Mwishehe (80)
aliyeangukiwa kichwani na ukuta wa
nyumba yake na kusababisha mauti yake.
Madhara mengine ni maji kujaa kwenye maeneo
mbalimbali, ikiwemo eneo la Mikocheni zilipo ofisi za Shirika la Umeme Tanzania
(Tanesco) Mkoa wa Kinondoni Kaskazini,
jirani na Hospitali ya TMJ, hivyo
kuleta usumbufu kwa wananchi wa eneo hilo na magari.
Kamanda Wambura alitoa mwito kwa
wananchi kuwa makini na kuchukua
tahadhari hususan kwa watoto, ambao hawawezi kujisaidia inapotokea mvua kubwa
kama hiyo, yenye kuhatarisha maisha.
“Kuna tabia ya kuwatuma watoto wadogo
dukani wakati mvua inanyesha, wazazi na walezi hii sio sawa, wanaweza kukutana
na maji mengi yakawazidi nguvu na kupoteza maisha, pia tuwe waangalifu na
maeneo ambako maji yanajaa, kwani wanaokatiza wanaweza kuzama,” alisema
Wambura.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala jijini
humo, Mary Nzuki alisema hali ni shwari
na hakuna tukio lililoripotiwa kwa muda huo. Aliwataka wananchi waishio
mabondeni, kuondoka mara moja badala ya kusubiri maafa.
“Nitoe rai kwa wakazi waishio
mabondeni, waondoke mara moja wasisubiri kuondolewa, na mvua hizi hazina hodi
na hatujui zitanyesha kwa kiasi gani na muda gani, ni vyema wachukue tahadhari
kwanza, maeneo hayo sio salama,” alisema Nzuki.
Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Temeke, Kihenya Kihenya
alisema hakuna tukio la maafa lililoripotiwa hadi muda huo na kuwataka wananchi
kuchukua tahadhari hasa kwa kipindi hichi cha mvua.
Mvua hiyo ilileta
kizaazaa kwa watumiaji wa vyombo vya usafiri na wakazi wote wa jiji baada ya
maji kujaa barabarani na kushindwa kufanya shughuli zao kwa wakati.
Mvua ilinyesha kwa saa muda wa saa mbili na
iliambatana na radi na upepo na kusababisha maeneo ya katikati ya jiji,
barabara zake kujaa maji, hali iliyosababisha usafiri kuwa mgumu. Aidha, mvua
hiyo ilisababisha wakazi wa jiji kusimamisha biashara zao kwa muda.
Katika Barabara ya
Bibi Titi Mohamed kuanzia maeneo ya Mnazi Mmoja, Akiba hadi Posta barabara hizo
zilijaa maji, hali iliyosababisha madereva wa magari madogo kushindwa kupita na
kuamua kutafuta njia nyingine huku magari ya Usafiri wa Dar es Salaam (UDA)
pekee ndio yalimudu adha hizo.
Pia katika maeneo
ya Posta kwenye kituo cha mafuta ya Total, karibu na Benki ya CRDB, kulijaa maji hivyo wafanyabiashara wa kituo
hicho kushindwa kutoa huduma ya mafuta kutokana na kutokuwepo kwa magari
yanayoingia katika kituo hicho.
Baadhi ya wakazi
wa jiji, walijawa na hofu kwamba kutokana na mvua kubwa iliyonyesha, itaweza
kusababisha madhara kwa watu waliokataa kuhama mabondeni.
Katika eneo la Posta Mpya, usafiri ulikuwa wa
shida, hali iliyosababisha watu kujaa
kwenye kituo cha daladala kwasababu magari
mengi yalikuwa hayafiki katika kituo hicho.
Baadhi ya watu walilazimika kuvua viatu
na kukanyaga maji machafu, yaliyokuwa yanapita barabarani huku wakilalamikia
ubovu wa miundombinu na kutokuwepo kwa mifereji.
Kutokana na maji mengi yaliyotuama
barabarani hasa katika eneo la Akiba, magari madogo yaliingia maji na kuzima
barabarani.
Mwandishi alilishuhudia gari dogo
likiwa limepaki karibu na Hoteli ya Holiday Inn huku dereva na abiria wake
wakichota maji kutoka kwenye gari na
kuyamwaga nje.
No comments:
Post a Comment