Mamlaka ya Hali ya Hewa nchini
(TMA) imesema msimu wa mvua za mwisho wa mwaka unaisha leo, ingawaje bado
inatarajiwa kuwa na mvua kuanzia mapema mwaka 2015.
Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dk Agnes Kijazi alisema
hayo Dar es Salaam wakati akizungumzia mvua iliyonyesha juzi na kusababisha
athari mbalimbali katika baadhi ya maeneo.
Akizungumzia mvua hiyo, Dk Kijazi alisema
ingawaje bado kuna mvua, lakini msimu wa mvua ulioanza Oktoba, Novemba na
Desemba unamalizika leo.
Alisema msimu huo, mvua haikunyesha kwa kiwango
kikubwa zaidi ya ile iliyonyesha juzi
kwa saa mbili katika jiji la Dar es Salaam.
Alisema kuwa mvua zinazotarajiwa kuanza mwanzoni
mwa Januari mwaka 2015, itakuwa nje ya msimu na inaweza kuwemo mvua kubwa pia.
Alisema mvua kwa mwezi wa Januari itanyesha kwa
wiki mbili na kuwataka wakulima kujiandaa kwa mazao, ambayo yataweza kupandwa
kwa kipindi hicho. Aliwataka wananchi kuwa na tabia ya kufuatilia taarifa za
mamlaka hiyo.
Mvua iliyonyesha juzi Dar es Salaam ilileta
athari mbalimbali ikiwa ni pamoja na vifo vya watu wawili katika maeneo tofauti
huku barabara zikijaa maji na kusababisha watu kushindwa kufanya kazi zao kwa
wakati.
Hata hivyo, wakizungumzia athari zaidi kwa mvua
hiyo kwa nyakati tofauti, makamanda wa Polisi wa Mikoa ya
Kipolisi ya Ilala, Temeke
na Kinondoni walisema hadi jana hali ilikuwa shwari na hakuna athari nyingine
zilizoripotiwa kutokea.
No comments:
Post a Comment