HAKIMU AJITOA KESI YA UGAIDI YA SHEKE FARID

Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Hellen Riwa amejitoa kusikiliza kesi ya ugaidi inayomkabili kiongozi wa Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislamu Zanzibar (Jumiki), Shekhe Farid Hadi Ahmed na wenzake. 

  Hakimu Hellen alitangaza kujitoa kusikiliza kesi hiyo jana kutokana na uamuzi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam ulioamuru Mahakama ya Kisutu kusikiliza na kutolea uamuzi ombi, lililowasilishwa na Shekhe Farid na wenzake.
Akitangaza kujitoa jana Hakimu Hellen alisema: “Mahakama Kuu ndiyo ina uwezo wa kusikiliza kesi hii…kwa kuwa Mheshimiwa Jaji ni mkubwa, mimi binafsi siwezi, najitoa”.
Katika ombi lao, washitakiwa waliomba Mahakama ya Kisutu ifute mashitaka ya ugaidi dhidi yao, pia walihoji uhalali wa kushitakiwa Tanzania Bara wakati Zanzibar ni nchi ambayo ina Mahakama Kuu na kuomba wakashitakiwe katika sehemu walizokamatwa.
Hakimu Hellen alisema kwa mujibu wa sheria, ushahidi hautoki hewani, unatoka kwenye hati ya mashitaka na kwa maoni yake maelezo ya kesi yalikuwa sahihi, lakini alikuwa anashangaa kwanini washitakiwa waliletwa Tanzania Bara.
Hata hivyo, alisema baada ya kusoma Sheria ya Ugaidi aligundua wanaweza kushitakiwa sehemu yoyote na hati ya mashitaka imeeleza wazi kuwa wanadaiwa kufanya matukio katika maeneo ya Tanzania Bara.
Awali kabla Hakimu hajajitoa, upande wa Jamhuri ulidai hawakuridhika na uamuzi wa Mahakama Kuu na wameshawasilisha kusudio la kukata rufaa ili Mahakama ya Rufaa itoe ufafanuzi wa uamuzi huo lakini kwa sasa wapo tayari kutekeleza kilichoamuliwa.
Upande wa utetezi ulidai Mahakama imeelekezwa kutoa uamuzi wa hoja zilizotolewa Oktoba 19 mwaka huu na wakaomba hakimu ajitoe ili Hakimu mwingine asikilize hoja hizo kwa kuwa hakimu Hellen alishatoa uamuzi.
Hata hivyo, Wakili Kongola alidai hakuna sababu za msingi za hakimu kujitoa na kama ikiwa ni hivyo, watamaliza mahakimu wote wa mahakama hiyo.

No comments: