Taasisi ya kifedha inayojihusisha na utoaji wa mikopo ya
Bayport Tanzania, imempatia Sh milioni tatu mwanafunzi wa mwaka wa kwanza wa
Chuo Kikuu kishiriki cha Mkwawa (MUCE), Kennedy Kaupenda, kufuatia huduma mpya
ya Bima ya Elimu inayoendeshwa na taasisi hiyo nchini.
Huduma hiyo mpya ya Bima ya Elimu ya Bayport Tanzania
ilianza mapema mwaka huu kwa ajili ya kuwapatia fursa wanafunzi kuendelea na
masomo baada ya mzazi aliyejiunga na huduma hiyo kufariki dunia.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es
Salaam, Mratibu wa Bima ya Elimu inayotolewa na Bayport Tanzania, Ruth Bura
alisema, Kaupenda alitajwa kama mnufaika kwa mzazi wake aliyefariki dunia,
hivyo waliamua kumtafuta kwa ajili ya kumpatia mafao yake.
Alisema huduma hiyo ina vipengele vinne ambavyo ni
Bronze, Gold, Silver na Exucutive ambapo makato ya kila mwezi ya Bronze
ni Sh 2,500 huku fao lake likiwa ni Sh milioni 3, wakati makato ya Gold ni Sh
6,250 huku fao lake likiwa ni Sh 7,500,000.
Bura alisema kipengele cha Silver makato yake kwa mwezi
ni Sh 3,800 huku mteja akilipwa fao la Sh milioni 4,500,000 na kipengele cha
Executive kikihusisha makato ya Sh 9,000 na kumpatia mteja fao la Sh
10,800,000.
“Tunaamini kuwa huduma hii ni sehemu ya kuhakikisha kuwa
Watanzania wanawawekea ulinzi wa elimu watoto wao na yeyote wanayemchagua wao
ili hata wanapoachwa waweze kunufaika na elimu bila vipingamizi,” alisema.
Akizungumzia fao hilo, Kaupenda alisema hakuwa na imani
kuwa angesoma vizuri baada ya baba yake kufariki, ila baada ya kutafutwa na
Bayport na kutaarifiwa juu ya mafao hayo, amepata nguvu mpya.
“Nasikitika sana baba kwa kunificha juu ya kujiunga na
huduma hii sambamba na kuwa mkopaji wa Bayport, hata hivyo namshukuru kwa
sababu fedha hizi zimekuja kunipa mwanga mpya wa kuhakikisha kuwa nasoma kwa
bidii, nikiamini kiasi cha Sh milioni tatu kitaniweka katika wakati mzuri mno,”
alisema Kaupenda.
Mbali na huduma hiyo ya Bima ya Elimu kwa uwapendao, pia
Bayport inajihusisha na mikopo kwa watumishi wa umma na kampuni
zilizoidhinishwa, ambapo hivi karibuni walizindua huduma ya Mikopo ya Bidhaa,
ambapo bidhaa za bodaboda aina ya Lifan, Toyo na Boxer zinakopeshwa kwa wateja
wa Bayport Tanzania.
No comments:
Post a Comment