KRISMASI YASHEREHEKEWA KWA AMANI DAR

Hali ya usalama katika jiji la Dar es Salaam imeelezwa kuwa shwari katika sikukuu ya Krismasi huku ulinzi ukiimarishwa zaidi kuelekea mwisho wa mwaka.
Jiji hilo lenye mikoa mitatu ya Kipolisi ya Ilala, Kinondoni na Temeke, hakuna matukio makubwa yaliyojitokeza.

Wakizungumza na mwandishi, makamanda wa mikoa hiyo walisema kwa jumla hali ya usama ni shwari. Walisema licha ya watu wengi kujitokeza katika maeneo mbalimbali ya starehe,  polisi waliweza kudhibiti usalama.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Mary Nzuki alisema katika mkoa wake hali ilikuwa ni shwari kwa kuwa polisi walikuwa ni wengi kuhakikisha hakuna jambo baya linaloweza kutokea.
Alisema, usalama wa kutosha katika eneo lake, unatokana na wao kujipanga vizuri ili kuhakikisha watu wanasherehekea Krismasi kwa amani.
Aidha, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Camillius Wambura alisema kuna baadhi ya matukio madogo ya kawaida ambayo yalijitokeza lakini yalidhibitiwa.
Alisema matukio hayo, hayakusababisha uvunjifu wa amani au  madhara mengine yoyote.
"Hakuna taarifa zozote za matukio makubwa hata ajali ni magari kwa magari lakini hakuna ambayo imesababisha kifo, hali ya usalama ni ya hali ya juu sana na hii itaendelea mpaka kwenye sikukuu za mwaka mpya," alisema.
Alisema ufukwe wa Coco ndiyo huongoza kwa kujaa watu wengi na ndivyo ilivyotokea,  lakini askari pia walikuwa ni wengi  na hakuna tukio lolote lililojitokeza.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Temeke, Kihenya Kihenya alisema licha ya kuwa na kumbi nyingi za starehe, zilizokuwa zikipiga muziki na watu kujaa, hakuna taarifa za matukio ya uhalifu au ya vifo yaliyojitokeza.
Makanda hao walisema kuwa hali ya usalama itaendelea kuimarishwa katika kipindi chote na hasa kwa kuzingatia bado kuna sikukuu za Mwaka Mpya.

No comments: