WANAOANDIKA MANENO YA UCHOCHEZI KWENYE KUTA WASAKWA


Watu wasiofahamika, usiku wa kuamkia jana wameandika maneno kwenye kuta ikiwamo ukuta wa Kampuni ya Bakhressa katika maeneo ya Tazara wakidhihaki Katiba Inayopendezwa sanjari na aliyekuwa Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba.
Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, imesema inafuatilia kubaini watu wanaoandika maneno ya uchochezi kwenye kuta na kwamba wakigundulika watashitakiwa kwa uchochezi na uvunjifu wa amani.
Miongoni mwa maandishi kwenye kuta hizo, yalitaka ipigwe kura ya hapana kwa Katiba Inayopendekezwa na kwamba ni mbovu. Mengine yalimshutumu Mwenyekiti wa Bunge hilo, Samuel Sitta.
Kamanda wa Polisi katika hiyo Maalumu, Suleiman Kova alisema wanaendelea kuwatafuta ili kuweza kuwabaini na kuwafikisha mahakamani. Alisisitiza jamii kutumia njia mwafaka ya kufikisha mawazo yao.
Alisema kwa kutoa maoni kwenye kuta hayana thamani, kwani hakuna atakayefanyia kazi lakini kwa kufuata taratibu yataheshimiwa.
Kutokana na maandishi hayo yaliyokutwa jana asubuhi, wafanyakazi wa kampuni hiyo ya Bakhressa walilazimika kuyafuta kwa kupaka rangi upya kwenye ukuta huo.
Mmoja wa vijana waliokuwa wakifuta maandishi hayo aliyejitambulisha kwa jina moja la Hassan, alisema baada ya uongozi kupata taarifa ya kuwepo maandishi hayo waliwataka kufuta na kupaka rangi upya.
Hivi karibuni, iliripotiwa kwamba mkoani Dodoma, maandishi kama hayo yalikutwa katika ukuta wa ofisi za Makao Makuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).

No comments: