WANAFUNZI ELIMU YA JUU WAKOPESHWA SHILINGI TRILIONI 1.8


Serikali imetoa Sh trilioni 1.8 kwa Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu nchini (HESLB) tangu kuanzishwa kwake kama mikopo kwa ajili ya wanafunzi wa elimu ya juu.
Mkurugenzi wa Elimu ya Juu, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya ufundi, Profesa Sylivia Temo alisema hayo jana Dar es Salaam na kuongeza kuwa pamoja na kiwango hicho bado  Bodi ya Mikopo imekuwa ikilalamikiwa.
Alisema Serikali imejenga mradi wa sayansi na teknolojia ambao kwa kiasi kikubwa utakapunguza gharama za  udahili kwa wanafunzi wa elimu ya juu ambapo kwa kiwango kikubwa utaondoa lawama zinazoelekezwa katika bodi hiyo.
“Kila mwaka Bodi ya Mikopo ya Elimuya Juu imekuwa ikilalamikiwa…tunaomba msaada kwa binafsi kujitokeza na kukopesha wanafunzi hao ili kupunguza lawama zinazoelekezwa kwa Bodi,” alisema.
Alisema kila mwaka serikali hutoa Sh bilioni 306 kwa ajili ya kukopesha wanafunzi wanaojiunga na elimu ya juu, fedha ambazo hazitoshi hivyo ni vyema taasisi nyingine zikaona suala hilo na kujitokeza ili kukabiliana na hali hiyo.
Alisema Serikali imekuwa na vipaumbele vingi ambapo haviwezi kwenda  pamoja kwa wakati mmoja jambo ambalo linaweza kuwa chanzo cha kuongeza lawama kwa Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu.
Kuhusu udahili alisema mradi wa sayansi na teknolojia utasaidia kupunguza gharama za udahili kwa mwanafunzi anayekwenda  kusoma chuo kikuu  kwa kuanza kupeleka taarifa zake Tume ya Vyuo Vikuu (TCU)    ambapo utakuwa ni wa kielektroniki.
Kadhalika alisema mfumo huo utasaidia wanafunzi wanaoomba mikopo ambapo utaweza kuchambua  ni mwanafunzi gani sahihi anayetakiwa na anahitaji kiwango gani ili kuweza kuendelea na masomo ya elimu ya juu.

No comments: