Wakati kundi la Umoja wa Katiba ya Wananchi
(Ukawa) likishinikiza Bunge Maalumu la Katiba lisitishwe haraka iwezekanavyo,
Bunge hilo limejiandaa kuwasilisha Katiba inayopendekezwa Septemba 21.
Hatua hiyo ya
Bunge Maalumu, inalenga kuwapa fursa wajumbe wa bunge hilo, kuipigia kura
Katiba hiyo.
Spika wa
Bunge hilo, Samuel Sitta alisema hayo jana. Aliongeza kuwa hatua hiyo
itadhihirisha kuwa kazi waliyopewa na taifa ya kuandika Katiba mpya, itakuwa
imekamilika.
Hatua hiyo ya
Bunge kufupisha ratiba zake, inatokana na uamuzi wa Serikali kuwa shughuli zote
za bunge hilo, ziwe zimekoma ifikapo Oktoba 4 mwaka huu na sio Oktoba 31.
Sitta
abainisha kuwa majadiliano ndani ya Bunge hilo yatakamilika kesho kutwa
Jumamosi na kuanzia Jumatatu ijayo kamati ya uandishi wa katiba, itaendelea na
kazi yake ambayo wataifanya kwa wiki moja na baada ya hapo watawasilisha
rasimu Septemba 21.
Ratiba
inafafanua kuwa baada ya katiba inayopendekezwa kuwasilishwa, wabunge
wataipitia kabla ya kuanza kupiga kura Septemba 26 mwaka huu.
“Nafurahi kuwaambia kwamba jana katika kikao
cha kamati ya uongozi, tumedhihirisha kwamba tunakwenda vizuri na kamati ya
uandishi, ambayo imekuwa ikitazama mambo yanavyokwenda na mjadala ulivyoanza
jana, tumejipanga kutupa rasimu ya mwisho tarehe 21 mwezi huu.
“Kwa hiyo ni
dhahiri kabisa kwamba lengo tulilopewa na taifa la kutoa katiba inayopendekezwa
tutalimudu ndani ya wakati huo,” alisema Sitta.
Sitta alisema
kwa sasa uongozi wa Bunge hilo, unaangalia utaratibu wa kupiga kura kwa
wale ambao wako nje ya Bunge kwa sababu mbalimbali ukiacha wale ambao walisusa
hasa wale ambao wako hospitali, ambao kanuni zinawaongoza utakapofika wakati wa
kupiga kura, waandaliwe utaratibu wa kufanya hivyo.
Alisema
wanafanya hivyo, kwa sababu akidi inahusu wabunge wote, ambao waliteuliwa na rais
kuwa wajumbe wa Bunge hilo na wajumbe wengine ambao wameingia kwa nyadhifa zao.
Upigaji kura
huo, pia utawahusisha wajumbe wa Bunge hilo ambao watakuwa safari nje ya nchi.
Baadhi ya wajumbe wanaenda Hijja huko Mecca, Saudi Arabia.
Katika
kuhakikisha kuwa wajumbe wengi wanachangia ndani ya muda ambao wamepewa,
uongozi wa Bunge hilo ulitoa mwongozo wa namna ya kuchangia na Sitta aliwataka
wajumbe kuhakikisha wanafuata muongozo huo ili kuokoa wakati.
“Jana kidogo
tuliongelea lakini leo mtaona kuna muongozo tumeugawa, kila mmoja ahakikishe
anao kwa sababu kiti kitaangalia tunakaa ndani ya muongozo huo, kwa leo nadhani
na kesho kwa sababu mjadala tuukamilishe kufikia siku ya Jumamosi hii
inayokuja, kwa hiyo tutakuwa tunagawa miongozo hii kuwawezesha waheshimiwa
wajumbe kujua tunalenga wapi,” alisema Sitta.
Mwongozo
alioutoa jana ulihusu Sura ya 2,3,4,5 ambao uliandaliwa na sekretarieti.
Alisema mwongozo huo ni muhtsari wa maoni, ambayo yalitoka ndani ya
kamati zote 12. Alisema kwa hali hiyo mwenendo huo, hautaruhusu kuibua upya
mjadala uliokuwapo ndani ya kamati.
Sitta
alifafanua kuwa kuna masuala mbalimbali ambayo rasimu ilisema na muhtasari
kamati zilijielekeza na kufikia muafaka na sehemu hawakufikia muafaka.
Aliwakumbusha wajumbe hao kuwa ni kazi yao sasa kuboresha yale yaliyopo
kwenye mwongozo huo.
Sitta alisema
kuhusu mambo ya imani ya dini, kamati kadhaa zilisema ibara hiyo ibaki kama
ilivyo kwenye rasimu ya katiba na nyingine zikaongezea kwamba uwepo
utaratibu wa kutambua na kuruhusu sheria na vyombo vya dini, kutambuliwa
kisheria.
“Sasa mjadala
wa jana ulifikia mahali kwamba kidogo uharibu mambo kwa sababu tumerejea tena
kuidai mahakama ya kadhi ndani ya katiba na wengine wanasema ndivyo ilivyo
Uganda wakati sio kweli, Zanzibar sio kweli mahakama kama hiyo inatambuliwa
ndani ya sheria, sio lazima ndani ya katiba.
“Tunachotunga hapa ni kuandika katiba, sio
sheria na kwa suala hili hapa kwa Tanzania Bara Kamati ya Pamoja ambayo
inasimamiwa na waziri mkuu imekuwa ikilishughulikia ili lifike mwisho wake, kwa
hiyo kulirejea tena na kusema kwamba ni jambo ambalo linazungumzwa ndani
ya katiba sio sahihi,” alisema Sitta.
Kwa hali hiyo
aliwaomba wajumbe, kuhakikisha kuwa hawarudii tena yale waliyoyajadili kwenye
kamati. Alisema kama hoja ilishindikana na ikawekwa pembeni, kutokana na
wajumbe kutofikia muafaka fulani; sio wakati wa kurejesha jambo hilo ndani ya
Bunge, kwani kufanya hivyo ni kuanzisha upya mjadala wakati kazi yao kwa
sasa ni kuboresha kile ambacho kinaweza kuleta muafaka.
Kutokana na
msimamo huo wa Sitta, baadhi ya wajumbe walimpinga na mjumbe wa kwanza kufanya
hivyo, alikuwa ni Ezekiah Oluoch aliyetaka apewe mwongozo, kwa sababu kuna
kifungu cha kanuni kinachotoa fursa kwa mjumbe yeyote wakati wa mjadala,
kuwasilisha marekebisho na maboresho au mabadiliko, ikiwa ni marekebisho
madogo, ambayo hayabadilishi msingi au maana.
“Kwa hiyo
mheshimiwa mwenyekiti tukiendelea tu na haya ambayo yamewekwa na kamati na
tusiongezee vingine, tutakuwa na shida kwa sababu tayari ulishapokea malalamiko
kwamba baadhi ya kamati hawakuweka hata vile vifungu, ambavyo vilikuwa
vimekubalika, kwa hiyo nilikuwa naomba nipate muongozo kwamba kwa nini hiyo
haki mjumbe asiitumie iliyopo kwenye rasimu na badala yake tutumie muongozo
tuliogaiwa asubuhi ya leo?” alihoji Oluoch.
Akijibu hoja
hiyo, Sitta alisema hilo ni jambo ambalo lipo wazi. Alionya kuwa taratibu wa
kuleta mabadiliko ni kitu kimoja, ambacho kitafumbua mjadala upya.
Alisema
mjadala huo ni kitu kingine na mambo yaliyokuwa ndani ya kamati ni kitu
kingine. Alisema yeye anajielekeza kwenye hilo la pili kuanzisha mjadala,
ambao tayari kwenye kamati walishazungumza.
Mwenyekiti
huyo alisema fursa za kuleta mabadiliko kwa maandishi, zinabaki palepale na
hata hatua ya kusoma ile rasimu kamili kuanzia ibara ya kwanza hadi ya mwisho,
ipo pale pale kwa mjumbe kuweza kupeleka pendekezo la mabadiliko ambalo
linaweza kupigiwa kura.
“Kwa hiyo
mimi sioni kama hayo mambo mawili yanapishana, hata kidogo, kuna kanuni za
mjadala ambazo lazima tuzizingatie, hatuwezi kurudia kazi tulizofanya kwenye
kamati kwa takribani wiki tatu tukairejesha kwenye mjadala, lakini kuleta
mapendekezo ya mabadiliko inaruhusiwa,” alisema.
Waziri katika
ofisi ya Rais asiyekuwa na Wizara Maalumu, Profesa Mark Mwandosya alionya kuwa
wajumbe walioko nje ya Bunge, ambao wanatarajia kuwa kuna katiba nyingine
itaandikwa baada ya mwaka 2015, wamechelewa.
Alisema
propaganda wanayoiendesha nje ya Bunge hilo kuwa mchakato huo utaanza
upya, hauna tija. Aliwahakikishia wananchi kuwa wajumbe wa bunge hilo,
wamefanya kazi kwa weledi mkubwa na watawapatia wananchi katiba mpya.
Wakati huo
huo, viongozi wa Ukawa waliitisha
mkutano na waandishi wa habari, Dar es Salaam
jana na kuendelea kumshinikiza Rais Jakaya Kikwete, atoe agizo mara moja
la kusitishwa kwa vikao vinavyoendelea vya Bunge Maalum la Katiba.
Aidha umoja
huo umependekeza katika Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ya mwaka 2013, ifanyiwe
marekebisho na kuwekwa kipengele kitakachotoa amri kwa utawala ujao,
kuhakikisha unamalizia mchakato wa Katiba uliositishwa kwa kuendelea na hatua
ya Bunge la Katiba.
Mwenyekiti
Mwenza wa umoja huo, James Mbatia alisema katika mazungumzo yaliyofanyika hivi
karibuni kati yao na Rais Kikwete, walikubaliana mchakato huo wa Katiba kwa
sasa usitishwe.
“Tumeshakubaliana
kimsingi kwamba mchakato huu wa Katiba hautaweza kufikia hatua ya mwisho kwa
wakati huu ya uchaguzi, muda umekwenda sana na makubaliano hayo tumetiliana
saini wote hadi wenzetu wa CCM, ila tunashangaa kwanini Bunge hilo hadi sasa
linaendelea tena hadi Oktoba 4, haya ni matumizi mabaya ya fedha za umma,”
alisisitiza Mbatia.
Alisema
katika makubaliano waliyoyafikia kwenye vikao hivyo, vilivyofanyika Agosti 31
na Septemba 8, mwaka huu, yalizingatia maoni ya wadau na kukubaliana kwa pamoja
kuahirisha mchakato wa katiba ili kupisha maandalizi ya Bunge la kawaida.
“Hata hivyo,
pamoja na makubaliano haya, sisi kama Ukawa msimamo wetu ni Bunge linaloendelea
la Katiba lisitishwe ili tuanze kufanyia marekebisho Katiba ya sasa tuweze
kufanya uchaguzi kwa maridhiano na amani,” alisema.
Alimpongeza
Rais Kikwete kwa kuchukua uamuzi wa kukubali kukutana na umoja huo kwa
mashauriano hadi kufanikisha, hatua hiyo
aliyoiita nzuri ya kuwezesha kupata muafaka wenye maslahi mapana kwa taifa,
kuhusu suala la katiba na uchaguzi.
Katibu Mkuu
wa Chadema, Dk Willibrod Slaa, alimtaka Sitta kuacha kutumia vibaya fedha za
umma na kusitisha mara moja Bunge hilo, vinginevyo kukitokea machafuko au
vurugu zinazotokana na mchakato huo wa Katiba atalaumiwa yeye.
Mwenyekiti
Mwenza wa Umoja huo kutoka CUF, Profesa Ibrahim Lipumba, alisema katika
marekebisho ya 15 ya Katiba ya sasa, walichopendekeza ni kuundwa kwa tume huru
ya uchaguzi, kuweka mgombea huru, Rais kuchaguliwa kwa zaidi ya asilimia 50 na
matokeo ya Urais kuhojiwa mahakamani.
Mwenyekiti wa
Chadema na Mwenyekiti mwenza wa Ukawa, Freeman Mbowe, wakati akifungua uchaguzi
wa Baraza la Vijana wa chama hicho Dar es Salaam jana, alisisitiza juu ya Bunge
hilo kusitishwa mara moja kabla ya Oktoba 4, mwaka huu, vinginevyo wataingia
barabarani.
No comments:
Post a Comment