DAWA ZA KUONGEZA UCHUNGU NI HATARI KWA WAJAWAZITO



Matumizi ya dawa za kienyeji kwa ajili ya kuongeza uchungu na kujifungua mapema, imeelezwa kuchangia zaidi vifo kwa wajawazito.
Mganga Mkuu wa Mkoa Kigoma, Dk Leonald Subi alisema hayo mjini Kigoma kwenye kikao cha wadau wa afya.
Kikao hicho kilihusisha kufanya tathmini na kuona hatua za kuchukua kukabiliana na vifo vya wajawazito na watoto wakati wa kujifungua mkoani humo. Kiliitishwa na shirika la Wolrd Lung Foundation.
Dk Subi alisema kuwa licha ya jitihada mbalimbali zinazofanywa na serikali kwa kushirikiana na wadau wengine, kukabiliana na hali hiyo, bado wajawazito wanajifungulia majumbani na kutumia dawa hizo hatarishi kwa maisha yao.
Alisema kumekuwa na upungufu wa vifo vya wajawazito na ongezeko la vifo vya watoto.
Alisema vifo vya wajawazito vimepungua kutoka vifo 74 mwaka 2009 hadi kufikia 49 kwa mwaka jana huku vifo vya watoto wachanga vikiongezeka kutoka 720 mwaka 2009 na kufikia 840 mwaka jana.
Mkurugenzi wa Miradi wa World Lung Foundation, Dk Nguke Mwakatundu alisema shirika lake linaboresha huduma za mama na mtoto mkoani humo, lakini changamoto ya vifo vya wajawazito ni kubwa, kutokana na kujifungulia majumbani.

No comments: