HAWA NDIO WATAKAOCHEZESHA MECHI ZA LIGI KUU YA VODACOM


Ikiwa imebaki siku moja kufunguliwa kwa pazia la Ligi Kuu Tanzania Bara msimu wa 2014-15, mambo tayari yamenoga baada ya kukamilika kwa safu ya waamuzi watakaochezesha mechi za ufunguzi wiki hii.
Ofisa Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi Tanzania, Silas Mwakibinga aliliambia gazeti hili jana, orodha ya waamuzi iko tayari na kuwataka watakaochezesha katika michezo hiyo kutenda haki.
Katika mchezo wa Yanga dhidi ya Mtibwa Sugar ya Mvomero, Morogoro, mechi itakayopigwa kwenye Uwanja wa Jamhuri itachezeshwa na mwamuzi Dominick Nyamisano kutoka Dodoma.
Wakati huo, mabingwa watetezi, Azam FC itakuwa mwenyeji wa Polisi ya Morogoro kwenye Uwanja wa Azam Complex Chamazi, Dar es Salaam katika mchezo utakaochezeshwa na mwamuzi Abdallah Kambuzi kutoka Shinyanga.
Mwamuzi wa Dar es Salaam, Hashim Abdallah atakuwa kwenye Uwanja wa Kambarage mkoani Shinyanga kuziamua timu mbili ngeni katika ligi msimu huu, wenyeji Stand United na Ndanda FC ya Mtwara.
Mchezo mwingine utakuwa ni kati ya Mgambo JKT ya Tanga dhidi ya Kagera Sugar ya Bukoba utakaochezwa kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga na kuchezeshwa na mwamuzi Kennedy Mapunda wa Dar es Salaam.
Aidha, Ruvu Shooting ya Pwani itacheza na Tanzania Prisons ya Mbeya kwenye Uwanja wa Mabatini, Mlandizi na kuchezeshwa na mwamuzi David Paulo wa Mtwara.
Washindi wa tatu wa ligi hiyo msimu uliopita, Mbeya City itawakaribisha JKT Ruvu ya Pwani kwenye Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya katika mchezo utakaochezeshwa na Mohamed Theophil wa Morogoro.
Baada ya michezo hiyo ya Jumamosi katika mchezo wa Jumapili, Simba watakuwa ni wenyeji wa Coastal Union ya Tanga kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, na mwamuzi Jacob Adongo wa Mara atachezesha.
Kwa mujibu wa Mwakibinga, waamuzi hao wa kati ni miongoni mwa waamuzi wa kati 21 watakaochezesha ligi hiyo iliyopangwa kufikia tamati Aprili 18, mwakani. Kutakuwa na waamuzi wasaidizi 46.
Mwakibinga alisema anategemea waamuzi hao watachezesha mchezo huo kwa kufuata sheria 17 za soka bila kupendelea na kwa haki.
“Hiyo ndio orodha ya kwanza, kuna nyingine itatoka kwani wapo wengi, na wasaidizi wao tayari, tuna imani watazingatia maadili ya kazi yao,” alisema Mwakibinga.

No comments: