WATOTO 100 KUFANYIWA UPASUAJI WA MOYO INDIA

Watoto 100  wenye maradhi ya moyo, wanatarajiwa kwenda India kwa matibabu ya moyo, ukiwemo upasuaji baada ya kufanyiwa uchunguzi katika hospitali ya Regency  jijini Dar es Salaam.
Kambi ya uchunguzi itafanyika mwezi huu. Imeandaliwa kwa pamoja na Hospitali ya Regency Klabu ya  Lions ya Dar es Salaam (HOST) and Fortis Escorts Heart Institute ya India.
Taarifa iliyotolewa na Hospitali ya Regency, ilisema kambi hiyo itakayofanyika katika hospitali hiyo kuanzia Agosti  11 na 12 mwezi huu, itaendeshwa na mtaalamu bingwa wa maradhi ya moyo kutoka Fortis Escorts Heart Institute ya India, Dk Ashutosh Marwah
“Uchunguzi utakaofanywa na mtaalamu huyo, utaangalia watoto wote wenye matatizo ya moyo, yakiwemo matundu na valvu na uchunguzi utafanyika katika hospitali ya Regency Upanga hivyo ni fursa kwa wenye matatizo ya moyo waje kuchunguzwa na mtaalamu kutoka India,” ilisema taarifa iliyotolewa na Mratibu wa maradhi ya moyo katika Klabu ya Lions, Dk Rajni Kanabar.
Dk Kanabar alisema uchunguzi wa moyo, pia utafanyika Zanzibar kuanzia Agosti 13 na 14. Aliomba Watanzania wote kuchangamkia fursa hiyo ili wajue matatizo yanayowakabili, watakapokutana na wataalamu.
Alisema wagonjwa 100 watachaguliwa kwenye kambi hiyo kwa ajili ya kwenda kufanyiwa matibabu na upasuaji nchini India kwa punguzo kubwa la gharama, wakati wengine watafanyiwa bure.
Alisema watoto wote watakaochaguliwa kwenda kwa matibabu nchini India, watasafiri kwa pamoja kwa ndege ya Shirika la Ndege la Emirates kati ya  Novemba na Desemba mwaka huu, kwenda kutibiwa katika hospitali kubwa na za kisasa nchini India.
”Katika kusherehekea miaka 50 ya Uhuru wa Tanganyika na Zanzibar, watoto 50 watachaguliwa kutoka Tanzania Bara na watoto 50 kutoka Tanzania Visiwani wakiwa na wasaidizi wao watasafiri na wanachama wachache wa Lions na wauguzi kutoka Regency Medical Center kwenye ndege ya matumaini,” alisema Dk Kanabar.
Kwa upande wake, Shiraz Rashid ambaye anasimamia michango ya kupeleka wagonjwa nje ya nchi, alisema mwezi Oktoba watafanya harambee kubwa kwa ajili ya kupata fedha za kuwapeleka watoto 100 India kwa ajili ya upasuaji.

No comments: