HATARI!! HOMA YA INI INAUA ZAIDI KULIKO UKIMWI

Idara ya afya mkoani hapa imehadharisha jamii dhidi ya ugonjwa wa ini, ikisema ni mbaya zaidi ya virusi vya Ukimwi.
Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Emmanuel Mtika alitoa hadhari hiyo kwenye kikao cha 27  cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC), mwishoni mwa wiki mjini hapa.
Alikuwa akiwasilisha taarifa ya hali ya upatikanaji wa  damu salama  katika  vituo,  vinavyotoa  huduma ya afya mkoani humo.
Alisema virusi vya  homa ya ini viligunduliwa kwenye damu, iliyokusanywa  kutoka kwa watu wanaochangia damu kwa  hiari yao, kuokoa maisha  ya wahitaji  wakiwemo wajawazito na watoto.
“Idara ya Afya imekumbana na  changamoto  kubwa  ya magonjwa  yanayoambukizwa  kwa njia  ya  damu  hususani homa ya ini,  kama iliyogunduliwa  kutoka  kwenye damu iliyokusanywa  kutoka kwa wateja,” alisema.
Alisema magonjwa  yanayoambukizwa kwa njia ya damu yaliyogundulika kwenye damu iliyokusanywa ni  homa ya ini aina  ya HBV.
Kwa mujibu wake,   asilimia 10.3  ya  watu 206   waliopimwa walikutwa na maambukizi  ya aina hiyo HBV, wakati aina  nyingine  ya homa ya ini ya HCV ambapo  ni asilimia  1.5 ya watu 30 walikutwa  na maambukizi ya ugonjwa huo.
Kwa upande  wa maambukizi  ya virusi vya Ukimwi,  ni asilimia 1.2 ya watu 28 waliopimwa na kukutwa na maambukizi hayo.
Akitoa mfano wa  upatikanaji hafifu  wa damu salama katika vituo vinavyotoa  huduma ya afya  mkoani humo,  alisema mahitaji ni chupa za damu  4,350 kwa mwaka. Lakini,  ni chupa 2,003 tu zilizokusanywa mwaka jana,  ambazo ni sawa na asilimia 53 ya mahitaji halisi.
“Hata  hivyo  ni  chupa za damu zipatazo 1,665 tu  zilizosambazwa  katika  vituo  vitano vinavyotoa huduma  ya afya  mkoani kwetu…hiki ni kiwango kidogo sana  ikilinganishwa na mahitaji  halisi,” alisema.

No comments: