WATANZANIA WATAKIWA KUKUZA KISWAHILI



Watanzania wametakiwa kuunga mkono kwa kuendeleza juhudi za waasisi wa makuzi ya lugha ya Kiswahili.
Hayo yalisemwa juzi na Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Eckenforde cha Jijini Tanga, Profesa Joshua Madumulla wakati wa uzinduzi wa Chama cha Lugha na Fasili ya Kiswahili Tanzania (Chalufakita) uliofanyika katika Chuo Kikuu cha Mtakatifu John mjini hapa.
Profesa Madumulla alisema kuna kila sababu za kuunga mkono kwa kuendeleza juhudi za waasisi wa makuzi ya lugha ya Kiswahili, wakiwamo Shaaban Robert, Shekhe Amri Abeid Kaluta, Mathias Mnyampala, Saadan Kandoro, Muhammed Said Abdulla, Akilimali Snowwhite na wengine.
Pia, alitaka kutambuliwa na kuheshimiwa kwa lugha na fasili ya Kiswahili ikiwa ni pamoja na kuenzi kazi zilizofanywa na waasisi wa makuzi ya lugha hiyo na kuyaheshimu makazi yao ya muda mfupi na mrefu.
Bado hatujawaheshimu vya kutosha tukiwalinganisha na wenzao wa ngambo, alisema Profesa Madumulla.
Alisema jambo la msingi ni kutaka kutambulisha nguvu na uwezo wa Kiswahili katika vipengele mbalimbali vya kijamii huku kipengele cha elimu na taaluma kikiwa mstari wa mbele katika kutiliwa mkazo.
Hakuna somo katika dunia hii lisilotumia lugha katika kufunzwa kwake iwe lugha ya sauti ama ya ishara kwa sasa tumekuza mno ugumu wa masomo hayo kiasi kwamba tunatanua bila kujitambua ugumu wa masomo, alisema Profesa Madumulla.

No comments: