WAJENZI WA BOMBA LA GESI WATOA BOTI YA WAGONJWA



Kampuni ya Maendeleo ya mafuta ya China (CNPC) inayosimamia ujenzi wa bomba la gesi kutoka Mtwara - Dar es Salaam imetoa msaada wa boti ya kubeba wagonjwa kwa wananchi wa kisiwa cha Songosongo kilichopo Kilwa mkoani Lindi.
Pia wametoa msaada wa viatu jozi 240, jezi za mpira 30 pamoja na mipira 10 kwa ajili ya mpira wa miguu kwa shule ya msingi Songosongo, vyote vikiwa na thamani ya dola za Marekani 65,000 (Sh milioni 105).
Akikabidhi msaada huo, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa kampuni hiyo, Mao Qiping alisema misaada hiyo ni shukrani kwa wakazi wa kisiwa hicho kwa ukarimu waliouonesha tangu walipoanza kazi ya ujenzi wa bomba hilo mpaka sasa linapotarajia kukamilika.
Alisema urafiki kati ya nchi hiyo na Tanzania ni wa muda kuanzia ujenzi wa reli ya TAZARA mpaka sasa wanapojenga bomba hilo ambalo ni mkombozi wa tatizo la umeme nchini jambo litakalosaidia kuinua uchumi wa nchi.
Akishukuru kwa msaada huo mara baada ya kukabidhiwa Mwenyekiti wa kijiji hicho, Abdallah Yahya  alisema msaada huo utasaidia kuwa na usafiri wa uhakika kwa wagonjwa kutokana na sasa kutumia mashua ambazo ni hatari kwa maisha.
Jambo lililoungwa mkono na Mwalimu Mkuu Msaidizi wa shule ya Msingi Songosongo, Haji Njechele alisema boti hiyo itasaidia kupunguza vifo ambavyo vilikuwa vikitokea kutokana na kukosekana usafiri.

No comments: