VIJIJI VITANO KULIPWA FIDIA MILIONI 287/- ZA UHARIBIFU WA WANYAMA



Serikali imetenga jumla ya Sh milioni 287 kuwalipa fidia wananchi wa vijiji 5 karibu na hifadhi ya wanyama Serengeti upande wa Wilaya ya Tarime mkoani Mara.
Fidia hiyo inatokana na uharibifu uliofanywa na wanyamapori kwa mazao yao shambani.
Vijiji vinavyohusika ni pamoja na Nyarukoba, Nyanungu , Gorong'a , Kemambo na Kegonga.
Kauli hiyo imetolewa na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Tarime Silvanus Gwiboha wakati akijibu maswali ya madiwani kuhusiana na suala la fidia kutoka serikalini baada ya tembo kufanya uharibifu mkubwa katika mashamba ya vijiji hivyo.
Katika kikao cha Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya Tarime  kilichofanyika hapo Agosti 27 katika ukumbi wa Halmashauri hiyo chini ya Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo Selvester Kisyeri Kaimu Mkurugenzi huyo alisema fedha hizo zilipatikana kutokana na juhudi kubwa ya Mbunge Nyambari Nyangweni aliyewasilisha suala hilo bungeni na Serikali kutoa ahadi ya kulipa fidia.
Mkurugenzi huyo alisema kitu wanachofanya sasa ni kuhakiki majina kwani yapo madai kuwa kuna watu wanafanya hila ya kudhulumu Serikali kwa kuandikisha majina hewa.
Wakati huo huo Baraza la Madiwani limewataka maofisa wa Kilimo kukabiliana na ugonjwa wa mnyauko na kubabuka mazao ya mahindi.
Ugonjwa huo umebainika kuwapo katika kata zaidi ya 15 za Nyarero, Nyanungu, Kitare, Turwa , Pemba , Nyamaraga , Nyandoto, Nyamisangura, Kibasuka, Nyakonga, Kemambo, Nyamwaga na Mbogi .
Imedaiwa kwamba ugonjwa huo umeathiri  asilimia 25 ya zao la mahindi.

No comments: