TANZANIA YAPOTEZA SHILINGI TRILIONI MOJA KILA MWAKA



Tanzania imekuwa ikipoteza tani 18 za dhahabu kila mwaka, zenye thamani ya zaidi ya Sh trilioni moja, kutokana na ujanja wa wawekezaji katika uchimbaji wa madini.
Imeelezwa kuwa watu hao huenda kinyume na taratibu za wachimbaji wadogo, katika kuchimba na kuuza madini hayo wakifanya hivyo kwa hila bila kutambuliwa rasmi.
Kauli hiyo imetolewa na Kamishna wa Madini Tanzania, Paul Masanja, ambaye aliongeza kuwa utaratibu huo unaotumiwa na wawekezaji ni wa kienyeji na unalitia Taifa hasara kubwa kutokana na madini mengi kupotea.
“Pamoja na wachimbaji hawa kulaliwa na wanunuzi wajanja kutokana na kutojua bei halisi ya madini, pia wamekuwa wakisababisha upotevu mkubwa wa madini yetu, ambapo kwa upande wa dhahabu jumla ya tani 18 hupotea kutokana na utaratibu huo wa kienyeji,” alisema Masanja.
Alisema kutokana na hali hiyo, Serikali imeanzisha utaratibu wa kuwatambua rasmi wachimbaji wadogo kwa kuwapatia ruzuku za kujiendeleza kupitia vikundi ambapo hadi sasa wachimbaji 11 wameshapatiwa ruzuku hizo takribani dola 558,000. 
Aidha alisema kwa sasa Serikali haiwezi kuruhusu wachimbaji hao wadogo kuuza madini kwa kutumia dola ili wapate faida kama wanavyodai kwa kuwa kitendo hicho kitaiua Shilingi ya Tanzania. 
“Hata hivyo, hili ni soko huria hatuwezi kupangia mtu bei ya kuuza madini kwa kuwa kwa sasa tuna soko huria lakini ili nchi yetu iwe salama, madini hayafai kuuzwa kwa dola,” alisema Masanja. 
Hivi karibuni akiwa wilayani Mbinga, mkoani Ruvuma, baadhi ya wachimbaji wadogo walimtaka Katibu Mkuu, aingilie kati na kuwasaidia watambulike rasmi katika biashara hiyo ya madini ikiwa ni pamoja na kuruhusiwa kuuza madini hayo kwa dola za Marekani ili wapate faida.

No comments: