UDA, WAMILIKI WA DALADALA WAUNGANISHA NGUVU DART



Shirika la Usafiri Dar es Salaam (UDA) na  wamiliki wa daladala mkoa wa Dar es Salaam wameunganisha nguvu zao kwa pamoja kwa lengo la kuendesha mradi wa mabasi yaendayo kasi (DART).
Uamuzi huo ulifikiwa juzi katika mkutano wa wamiliki wa daladala Mkoa wa Dar es Salaam uliofanyika Ukumbi wa Karimjee, ukiwa umeandaliwa na kamati teule ya wamiliki wa daladala jijini.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti viongozi wa vyama vya wamiliki wa daladala vya DARCOBOA na UWADAR, Sabri Mabruki na William Masanja, walisema kuwa wameamua kuunganisha nguvu na UDA ili kuweza kumudu ushindani na makampuni makubwa yatakayokuja kutoka nchi zilizoendelea hususan Ulaya na Marekani katika mradi wa DART.
“Waswahili wanao msemo kwamba Umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu, hatuwezi kushinda zabuni ya kuendesha DART kama tutakwenda tukiwa tumegawanyika kama tulivyo sasa, yaani UDA kivyao na sisi DARCOBOA na UWADAR kivyetu hatufiki popote, DART itachukuliwa na wazungu,” walisema.
Wakitoa maoni yao kuhusu uamuzi huo baadhi ya wakazi wa Dar es Salaam wamewapongeza wamiliki wa daladala pamoja na UDA kwa kuunganisha nguvu zao kwa lengo la kumiliki uchumi wa nchi yao kama wazawa wa nchi hii.
 “Hii ni nzuri kwani tunakaribisha maendeleo kwa pamoja, suala la ubinafsi siku zote ndilo linalokwamisha ukuaji wa uchumi, hivyo basi ni wazi kuwa uamuzi huo licha ya kuwafaidisha wamiliki pia utawanufaisha na Watanzania wengine kwa kupata ajira na wakazi wa Dar es Salaam kuwa na usafiri bora,” alisema Rayness Tegemeo.

No comments: