REAL MADRID WAFANYA KWELI MBELE YA RAIS KIKWETE DAR



Magwiji wa Real Madrid wamethibitisha kuwa timu yao ndio miamba ya soka duniani, baada ya kuishinda timu ya Tanzania XI kwa mabao 3-1 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Mbele ya Rais Jakaya Kikwete, wachezaji hao wa zamani wa Real Madrid wakiongozwa na Luis Figo, walitandaza soka ya kuvutia na kuwafurahisha maelfu ya mashabiki wa soka.
Real Madrid kwa sasa ndio miamba ya soka Ulaya ikiwa imetwaa taji la 10 Mei mwaka huu, na miongoni mwa waliokuja, wamechangia katika kupatikana kwa mataji hayo muhimu.
Mchezaji Ruben de la Red alikuwa mwiba mkali kwa Tanzania XI ikiongozwa na wanasoka nyota wa zamani wa Tanzania, baada ya kufunga mabao yote matatu likiwamo la penalti.
Bao pekee la Tanzania halikufungwa na mchezaji wa nyota hao wa zamani wa Tanzania, bali alijifunga mchezaji wa Real Madrid.
Bao la Tanzania XI lilipatikana katika dakika ya 45, likifungwa na mchezaji wa Real, Roberto Rosas kutokana na kona iliyochongwa na Mecky Maxime kutoka mashariki mwa uwanja.
Madrid walijipatia bao la kuongoza katika dakika ya 15 likifungwa na Ruben de la Red kwa pasi ya nyota wa zamani duniani, Figo.
Hadi mapumziko, Tanzania XI na Real Madrid, zilikuwa sare ya bao 1-1.
Kipindi cha pili, Real Madrid iliendeleza kutandaza soka ya kuvutia huku Figo akiwa mwiba mchungu kwa Tanzania XI ambayo ilionekana kupwaya kipindi hicho.
Hali hiyo ilimpa mwanya De la Red kufunga bao la pili kwa penalti baada ya Habib Kondo na Mtwa Kihwelo, kumchezea dhambi mmoja wa wachezaji wa Real, mfungaji kupiga penalti nzuri iliyompita kipa Peter Manyika.
Kama hiyo haitoshi, mchezaji huyo alifunga bao la tatu baada ya kuwapiga chenga walinzi wa Tanzania XI na kipa wao Manyika, na kukwamisha mpira wavuni.
Bao hilo lilimfurahisha Rais Kikwete na viongozi wengine wa jukwaa kuu ambao walicheka sana kutokana na jinsi lilivyofungwa, huku wachezaji wa Tanzania wakiwa wameanguka chali.
Kipindi cha kwanza, Dua Said aliifungia Tanzania XI, lakini bao hilo lilikataliwa.
Mbali ya Figo aliyekuwa Mwanasoka Bora wa Ulaya mwaka 2000 na Mwanasoka Bora Duniani mwaka 2001, pia alikuwapo nyota Christian Karembeu katika kikosi cha Madrid.
Awali, Tanzania XI ilianza na kipa Mohammed Mwameja na miongoni mwa wachezaji waliocheza jana kwa upande huo, ni manahodha wa zamani wa Stars, Shadrack Nsajigwa, Mecky Maxime na Salum Sued ‘Kussi.’
Wengine waliocheza ni Yusuf Macho, Habib Kondo, Dua Said, Abubakari Kombo, Athumani China, Mtwa, Shaaban Ramadhani, Sabri Ramadhani, Kally Ongala, Madaraka Selemani, Stephen Nyenge, Mao Mkami, Emmanuel Gabriel, Nassoro Bwanga, Abdul Maneno.
Katika mechi hiyo, timu zilikaguliwa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo, Dk Fenella Mukangara, wakati Rais Kikwete alikuwa mgeni rasmi uwanjani hapo.
Mwishoni mwa pambano, alikabidhi kombe kwa De la Red na kisha akamkabidhi mpira kwa kufunga mabao matatu, huku akiweka saini yake.
Magwiji hao wa Real Madrid ambao wako nchini kwa mwaliko wa Kampuni ya TSN inayomilikiwa na Farough Baghozah, leo itakwenda mkoani Kilimanjaro kutembelea Mlima Kilimanjaro.
Kesho itakuwa mkoani Arusha katika mbuga ya Ngorongoro, na itarejea Dar es Salaam na kuondoka Jumanne ijayo kurejea makwao.

No comments: