SITTA ADAI KULIVUNJA BUNGE KWA SASA NI HASARA



Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel Sitta amesema Katiba ya sasa yenye miaka 50 imewezesha kutungwa kwa sheria  na kanuni zinazoleta maumivu kwa wananchi na kusema lengo la kutungwa kwa Katiba mpya ni kuziba mianya hiyo.
Alipinga kauli za baadhi ya wabunge wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) na wananchi wengine wanaotaka bunge hilo livunjwe kwa maelezo ya kuokoa fedha, akisema ni upuuzi kwani limeshafikia hatua ya mbali hivyo ni hasara kulivunja.
Sitta alibainisha hayo alipokutana na wakulima wa pamba kutoka mikoa 11 waliowasilisha kwake maoni ya wakulima wenzao wanayotaka yaongezwe kwenye majadiliano ya rasimu ya katiba yanayoendelea mjini hapa.
“Katiba tunayotengeneza lazima izibe mianya ya kuwaumiza wananchi na kuwadhibiti watendaji, mfano juzi Mwanza kuna wakulima wamekaa hapo tangu mwaka 1970 sasa wameondolewa kwa  kupigwa na kunyang’anywa nyavu zao. Lengo la kutungwa katiba mpya ni iwe rafiki kwa wananchi wa kawaida,” alisema.
Sitta alipoulizwa kama ni sawa kisheria Ukawa kutoshiriki Bunge la maalumu alijibu:
“Ukawa haijavunja sheria na si kosa kikanuni, siwezi kuwalaumu ila nyinyi wananchi pimeni, wametumia njia hiyo kuonesha hisia zao, lakini inaleta wasiwasi kuonesha sasa inakuwa tabia, kama unamuona mtu mpumbavu dawa si kususa ila muelimishe.”
“Wao wanaona roho ya katiba ni serikali tatu nasi tunaona roho ya katiba ni matakwa ya wananchi, sisi tuendelee kutunga katiba tuwaache wao wachache. Mwenye kujibu hili ni wananchi wenyewe si hao wanaojiona wana akili sana,” alisema.
Kwa upande wa Katibu Mkuu wa Chama cha Wakulima wa Pamba (Tacoga), George Mpandiyi  aliyesoma maazimio ya wakulima wa pamba, alisema wanataka vyama vya siasa vitambue wakulima wanataka Katiba mpya haraka itatue matatizo yao hivyo wamemtaka mlezi wa chama  chao, John Shibuda kuendelea kuhudhuria mjadala wa Bunge la Katiba.
Naye mwenyekiti wa chama hicho aliyeongoza msafara huo, Godfrey Mokiri alitaja maoni yanayotaka yaingizwe kwenye rasimu ya katiba kuwa ni Haki ya ardhi kwa wakulima na wafugaji ili kuzuia migogoro ya ardhi, haki za wakulima kupata mikopo, ruzuku za pembejeo kwa wakulima na katiba izuie dhuluma mbalimbali kwa wakulima na inapotokea walipwe fidia.

No comments: