HII NDIO ZAHANATI YENYE MGANGA MMOJA TU KWA MIAKA SABA



Zahanati ya kijiji cha Nafuba, kilichopo katika kisiwa ndani ya Ziwa Victoria wilayani Bunda mkoani Mara, ina mganga mmoja tu ambaye amekuwa akilazimika kuifunga anapopata dharura na kusababisha wagonjwa kukosa huduma ya matibabu.
Mganga Mkuu wa Zahanati hiyo Robert Magela, ameliambia gazeti ili juzi kuwa amekuwa akifanya kazi katika mazingira hayo kuanzia mwaka 2007 na kwamba yeye alihamia kwenye kituo hicho mwaka 2003 kukiwa na muuguzi mmoja ambaye pia baadaye aliondoka.
Alisema kuwa pindi anapopata dharura ama ya kuitwa wilayani kwa ajili ya kupeleka taarifa, amekuwa akiifunga zahanati hiyo hali ambayo husababisha wagonjwa kukosa huduma ya matibabu, wakiwemo akinamama wajawazito wanaotaka kujifungua.
“Nimefanya kazi hii nikiwa mwenyewe tangu mwaka 2007…nafanya huduma zote mimi mwenye na ninapopata dharura nimekuwa nikilazimika kuifunga, hali ambayo husababisha wagonjwa kukosa huduma” alisema.
Alisema zahanati hiyo inahudumia wananchi zaidi 4,493, wakiwemo wagonjwa  kutoka katika kisiwa hicho na kisiwa kingine jirani cha Sozia, ambapo wakazi wake wengi ni wavuvi na wafabiashara wa kutoka katika mikoa yote ya kanda ya ziwa.
Aidha, alisema kuwa hali hiyo imekuwa ikimfanya asipate nafasi ya kupumzika, kwani hali ya magonjwa katika kisiwa hicho iko juu, kulingana na mazingira halisi yalivyo visiwani humo, ambapo baadhi ya kaya hazina vyoo.
Mganga huyo ameiomba serikali pamoja na mashirika yasiyokuwa ya kiserikali yanayoshughulika na masuala ya ukimwi kufika katika visiwa hivyo, ili waweze kutoa elimu kwa jamii juu ya maambukizi ya ukimwi na jinsi ya kujikinga na ugonjwa huo hatari, badala ya elimu hiyo kuitoa sehemu za mjini tu.

No comments: