CHANA: TOENI TAARIFA ZA UKATILI WA KIJINSIA

Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Pindi Chana ameitaka jamii kutoa taarifa za ukatili wa kijinsia, badala ya kuona kama ni mila na desturi.
Chana alisema hayo jijini Dar es Salaam jana baada ya kutembelea kituo cha "One Stop", kinachohudumia watu waliofanyiwa ukatili kilichopo katika hospitali ya Amana pamoja na makao ya watoto Kurasini.
Alisema kuwa wapo watu wengi wanafanyiwa ukatili na jamii inafahamu lakini wanakaa kimya hawatoi taarifa kutokana na tamaduni mbalimbali.
"Matukio ya ukatili ni mengi katika jamii ila wakati umefika sasa wa kusema matukio hayo sasa basi. Tutumie vituo kama hivyo kutoa taarifa za ukatili ili na muathirika apatiwe huduma," alisema.
Alisema pia yapo madawati ya jinsia katika vituo vya polisi, hivyo jamii ihakikishe inavitumia ipasavyo na kuripoti matukio yote ya ukatili. Aidha, alisema jukumu la kuwatunza watoto ni la wote ili wasiishi mitaani, hivyo ukatili unatakiwa kukomeshwa.
Kituo cha One stop kilianzishwa Desemba mwaka jana. Hadi sasa kimewahudumia wahanga 293, ambao ni waathirika wa ukatili wa kijinsia na ukatili dhidi ya watoto chini ya miaka 18.
Mbali na kutembelea vituo hivyo,  pia Chana alitembelea Manispaa ya Temeke na kuzungumza na viongozi wake pamoja na kupokea taarifa ya Idara ya Maendeleo ya Jamii, Ustawi wa Jamii na vijana.

No comments: