SERIKALI YAMWAGA WATAALAMU KILA KONA KUKABILI EBOLA

Serikali kupitia Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imesambaza wataalamu wa afya katika mipaka yote nchini, ikiwa ni tahadhari ya kukabiliana na ugonjwa wa ebola.
Kusambazwa kwa wataalamu hao wa afya ni sehemu ya mikakati iliyowekwa na serikali kupitia wizara hiyo ya kuimarisha ufuatiliaji wa ugonjwa huo na kuhakikisha unadhibitiwa.
Msemaji wa wizara hiyo, Nsachris Mwamwaja alisema, wataalamu hao mbali na kusambazwa katika mipaka yote nchini lakini pia katika viwanja vya ndege vya kimataifa ili kuhakikisha watu wenye virusi vya ugonjwa huo wanajulikana kabla ya kuingia nchini.
Mwamwaja alisema mikakati mingine iliyopo ni kushirikiana na wadau mbalimbali, ikiwemo Shirika la Afya Duniani (WHO) na Kituo cha Kuzuia na Kudhibiti Maradhi cha Marekani (CDC) katika kukabiliana na ugonjwa huo.
"Pia kusimamia mpango mkakati wa kupambana na ebola ambao upo, maandalizi ya kudhibiti ugonjwa huu tulishayafanya mwaka 2012 wakati nchi jirani ya Uganda ilipopata wagonjwa wa ebola," alisema Mwamwaja.
Alisema wataalamu wa afya wataendelea kutoa elimu ya afya juu ya ugonjwa huo ambao alisema hauna chanjo wala tiba. Aidha, alisema mpaka sasa kwa hapa nchini hakuna mgonjwa aliyedhaniwa au kuthibitishwa kuwa na virusi vya ugonjwa huo.
Mwamwaja alisema wizara inawasihi na kuwaomba wananchi kutokuwa na hofu bali wachukue tahadhari za kujikinga na ugonjwa huo. Alisema wizara itaendelea kutoa taarifa juu ya ugonjwa na mikakati iliyopo ya kukabiliana nayo.
Ugonjwa huo wa ebola uliibuka hivi karibuni katika nchi ya Guinea na kusambaa katika nchi za  Sierra Leone, Liberia kati ya Julai 18 na 20, mwaka huu.
Tayari katika nchi hizo wagonjwa 1,323 wameripotiwa kukumbwa na ugonjwa huo huku vifo 729 vikiripotiwa.
Ugonjwa huo unaambukizwa kwa kugusa damu ya mtu mwenye ugonjwa huo au maji maji ya mwilini mwake, kugusa maiti ya mtu aliyekufa kwa ugonjwa huo.
Dalili za ugonjwa huo zimeelezwa kuwa ni kupatwa na homa kali ya ghafla, kulegea kwa mwili, maumivu ya misuli, kuumwa na kichwa pamoja na kutokwa na vidonda kooni.
Aidha, dalili hizo hufuatiwa na kutapita, kuharisha, kutokwa na vipele, figo na ini kushindwa kufanya kazi na kwa baadhi ya wagonjwa kutokwa na damu ndani na nje ya mwili.

No comments: