ASHIKILIWA KWA TUHUMA ZA MAUAJI

Mkazi wa Kata ya Busi Tarafa ya Pahi Wilayani Kondoa mkoani Dodoma, Bakari Hussein (30) anashikiliwa na Jeshi la Polisi kwa tuhuma za mauaji.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, David Misime alisema tukio hilo  lilitokea Julai 31, mwaka huu.
Alisema mtuhumiwa alimuua Rukia Juvency (50) kwa kumpiga mtama na alipoanguka alimpiga na tofali la saruji kichwani upande wa kushoto na kumsababishia kifo muda mfupi baada ya kufikishwa katika Kituo cha Afya cha Kijiji cha Busi.
Kamanda Misime alisema chanzo cha mauaji hayo kinachunguzwa, ingawa mtuhumiwa anadai siku ya Idd el Fitr alitukanwa na mwanamke huyo.
Aidha,  Kamanda Misime alisema mtuhumiwa amekamatwa na atafikishwa mahakamani baada ya taratibu kukamilika. Alitoa mwito kwa wananchi, kuacha kujichukulia sheria mkononi.
“Kama umetukanwa ufumbuzi wake ni kwenda kushitaki katika idara zilizowekwa kisheria ili walifanyie kazi tatizo hilo,” alisema.

No comments: