Waziri wa Fedha, Saada Mkuya Salum, anasubiriwa wiki hii
kutegua kitendawili cha hoja za wabunge, kuhusu punguzo la kodi katika
mishahara, vyanzo vipya vya mapato na
utekelezaji wa miradi wa maendeleo.
Leo ndio siku ya mwisho kwa wabunge kujadili hotuba ya
bajeti ya Waziri Saada na kesho Waziri
ataanza kujibu hoja akishirikiana na
Naibu wake, Mwigulu Nchemba na Adam Malima.
Katika majibu yake, Waziri Saada anatarajiwa kuonesha
namna Serikali ilivyojipanga kusimamia nidhamu ya makusanyo na matumizi ya
fedha za Serikali, ikiwemo hatua aliyoitangaza ya kufuta misamaha ya kodi isiyo
na tija.
Wabunge wengi, pamoja na kuipa Serikali changamoto,
walielezea kuridhika na utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika majimbo yao,
hasa miradi ya umeme vijijini na maji.
Pia ufikishaji wa bomba la gesi Dar es Salaam ni moja ya
miradi inayoipa Serikali sifa kwa kuwa matarajio ni Serikali kuacha kutumia
fedha nyingi katika ununuzi wa mafuta ya dizeli na petroli kwa ajili ya
uzalishaji umeme.
Aidha, bei ya nishati hiyo kutoka kwa kampuni zinazofua
umeme, inatarajiwa kushuka kutoka senti za Marekani 30 na 60 kwa uniti moja
mpaka chini ya senti 18 za Marekani kwa uniti moja na kusaidia Serikali kutekeleza
nia yake ya kushusha bei ya umeme.
Nafuu hiyo ya bei ya umeme, mbali na kuleta nafuu ya
maisha kwa mwananchi mmoja mmoja mijini mpaka vijijini, inatafsiriwa kuwa
kivutio cha uwekezaji, kitakachochangia ongezeko la ajira na ukuaji wa uchumi
wa nchi ambao kwa sasa ni asilimia saba.
Katika mijadala ya wabunge, wengi walipongeza hotuba ya
Bajeti na kutaka maoni ya Kamati ya Bajeti, inayoongozwa na Mbunge wa Bariadi
Magharibi, Andrew Chenge (CCM), yazingatiwe
kuboresha upatikanaji wa mapato.
Katika maoni ya Kamati hiyo, Chenge alisema upo udhaifu wa Serikali katika utekelezaji wa
bajeti, kutokana na kuendelea kutegemea vyanzo vile vile vya mapato, huku
matumizi yake yakiwa makubwa ikilinganishwa na mapato.
Akiwasilisha taarifa yake, Chenge alisema kamati yake
imeshitushwa na ukuaji wa deni la taifa, akisema ilo ni mzigo mkubwa. Alisema
hivi sasa deni hilo ni tishio kwa uchumi wa taifa.
“Serikali imeendelea kuja na vyanzo vile vile vya
kiutamaduni vilivyozoeleka, ambavyo ni pombe, sigara, vinywaji baridi na
vinywaji vikali, wakati kuna vyanzo vingine vingi,” alisema Chenge.
Alitaja baadhi ya vyanzo vipya ambavyo Kamati yake
inaamini vinaweza kuingizia Serikali mapato mengi, ni pamoja na uvuvi wa Bahari
Kuu, kupiga mnada vitalu vya misitu na uwindaji wa kitalii, kupiga mnada masafa
ya mawasiliano pamoja na kodi za majengo.
Kwa mujibu wa Chenge, Kamati yake inashangazwa na majibu
yanayotolewa na Serikali kuhusu suala la ukusanyaji wa mapato katika uvuvi wa Bahari
Kuu, kwamba haiwezi kukusanya hadi itakapojenga bandari
maalumu ya uvuvi.
“Kwa taarifa rasmi
za Serikali zilizotolewa bungeni, Serikali inapoteza takriban Dola za Marekani
milioni 222, sawa na Sh bilioni 372.9. Kamati inahoji hadi hapo tutakapojenga
bandari maalumu ya uvuvi, tutakuwa tumepoteza mapato kiasi gani,” alihoji.
Alisema Kamati yake imechambua bajeti ya mwaka 2013/2014
na kubaini kuwapo kwa madeni makubwa katika baadhi ya wizara na taasisi
mbalimbali za umma.
“Mfano Wizara ya Ujenzi imekuwa ikitekeleza miradi ya
ujenzi wa barabara bila kuwalipa makandarasi kwa wakati na kwa kuzingatia
mikataba yao na hivyo kujikuta ikianza kila mwaka wa fedha ikiwa na malimbikizo
makubwa ya madeni.
“Hali hii
imesababisha Wizara hii kutumia bajeti yake ya mwaka unaofuata kulipia madeni
ya mwaka uliopita, badala ya kutekeleza miradi iliyoidhinishwa kwa mwaka husika
wa fedha,” alisema Chenge.
Akizungumza kuhusu deni la taifa, Chenge alisema licha ya
Serikali kusema deni hilo ni himilivu, lakini kwa uhalisia deni hilo ni mzigo
mkubwa kwa taifa linaloathiri uchumi wa nchi.
“Hadi kufikia Machi 2014, deni la taifa linalojumuisha
deni la Serikali na deni la nje la sekta binafsi lilifikia Sh trilioni 30,
ikilinganishwa na Sh trilioni 23 mwezi Machi, 2013,” alisema.
Chenge alitoa sababu kadhaa zinazoifanya Kamati yake
ishindwe kukubaliana na hoja ya Serikali kwamba deni hilo ni himilivu.
“Mosi, kuna madai mengi ya ndani ambayo hayajajumuishwa
katika deni la taifa na taarifa zilizopo zinaonesha kuwa madai haya yanaendelea
kuongezeka.
Sababu nyingine ni kwamba, uwiano uliopo wa deni la taifa na pato la
Taifa kiuchumi si wa kuridhisha, ukubwa wa deni hili hauwiani na kiwango cha
uzalishaji na ukuaji wa uchumi wa sasa wa asilimia saba.
Pia alisema, udhaifu
katika usimamizi wa matumizi ya fedha za umma na ucheleweshaji wa uhakiki wa
madai ya ndani ni sababu nyingine. Taarifa ya Waziri wa Fedha ya nusu mwaka
inaonesha, malimbikizo ya madai hadi Desemba, 2013 yalikuwa yamefikia Sh
trilioni 2.09, ambayo ni asilimia nne ya
pato la Taifa,” alisema.
Wabunge wengi pia walisema punguzo la Kodi katika
Mshahara (Paye), kutoka asilimia 13 mwaka unaoisha wa fedha 2013/2014 mpaka
asilimia 12 kwa mwaka ujao wa fedha 2014/2015, kuwa ni ndogo.
No comments:
Post a Comment