WAWILI WAJITOKEZA KUMKABILI LIPUMBA UCHAGUZI MKUU CUF



Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF) Profesa Ibrahim Lipumba, na Katibu Mkuu wa chama hicho,  Seif Sharif Hamad bado wanahitaji kuendelea na nafasi hizo za uongozi kitaifa baada ya kuchukua fomu kuzitetea katika uchaguzi utakaofanyika wiki hii.
Katika mkutano huo mkuu wa sita wa chama hicho utakaofanyika jijini Dar es Salaam, viongozi hao, Lipumba na Hamad  wataachia ngazi kupisha uchaguzi mkuu kufanyika.
Katika hafla maalumu ya kuagana na wajumbe wa Baraza Kuu na watendaji wengine wa ngazi mbalimbali za chama hicho,  Lipumba aliahidi  kukubaliana na matokeo, iwapo atashindwa na kwamba ataendelea kuunga mkono chama hicho kwa kutoa kila msaada unaostahiki.
“Nilikuwa mwanachama wa kawaida kwa kipindi kirefu ndipo ikafika wakati chama kikaniteua kugombea na kuchaguliwa Mwenyekiti hadi leo, kwa hivyo haki hii anaweza kuwa nayo mwanachama yeyote”, alisema Lipumba katika hafla hiyo iliyofanyika nyumbani kwake.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa CUF, Hamad, alisema kila mwanachama ana wajibu wa msingi wa kukijenga chama bila kujali wadhifa alionao.
Katika hafla hiyo iliyofanyika nyumbani kwa Profesa Lipumba, Hamad alipongeza wajumbe wa Baraza kwa ushirikiano katika kipindi chote cha miezi 64, hali ambayo alisema imeleta mafanikio makubwa ndani ya chama.
Akizungumza namwandishi, Mkurugenzi wa Haki za Binadamu, Habari na Uenezi wa chama hicho, Salim Biman, alisema Lipumba anatetea nafasi ya uenyekiti, aliyoishika kwa zaidi ya miaka 10 sasa akipambana na wenzake wawili.  Alitaja wagombea wengine wa nafasi hiyo ni   Chifu Yemba kutoka Shinyanga na M’bezi Adam Bakar kutoka Temeke,  Dar es Salaam.
Katika nafasi ya Ukatibu Mkuu, Hamad  ni mgombea pekee wa nafasi hiyo huku nafasi ya Makamu Mwenyekiti wa chama hicho, ikiwaniwa na Juma Duni Haji ambaye  pia ni mgombea pekee.
Makamu Mwenyekiti wa Chama hicho, Machano Khamis Ali, amesema ameamua kwa hiari yake kutogombea tena, kutokana na sababu mbalimbali, zikiwemo za kiafya
Aidha, alisema katika uchaguzi huo, pia kuna nafasi 45 za ujumbe wa Baraza zinazowaniwa. Kati ya hizo,  20 ni wajumbe kutoka Zanzibar na 25 wajumbe kutoka Tanzania Bara na uchaguzi wa Viti Maalumu.
“Kesho (leo) tunatarajia kuanza mkutano mkuu wa sita  wa chama ambao kikatiba ndio mkubwa wenye maamuzi makuu ya mwisho ya mambo mbalimbali ndani ya chama, ikiwemo kupitisha wagombea wa nafasi mbalimbali katika uchaguzi wa ndani wa chama,” alisema Bimani.
Alisema mkutano huo wenye wajumbe zaidi ya 800 kutoka sehemu mbalimbali Bara na visiwani,  utafanyika kwa siku tano kuanzia leo  hadi Ijumaa, jijini Dar es Salaam.

No comments: