Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF) Profesa Ibrahim
Lipumba, na Katibu Mkuu wa chama hicho,
Seif Sharif Hamad bado wanahitaji kuendelea na nafasi hizo za uongozi
kitaifa baada ya kuchukua fomu kuzitetea katika uchaguzi utakaofanyika wiki
hii.
Katika mkutano huo mkuu wa sita wa chama hicho
utakaofanyika jijini Dar es Salaam, viongozi hao, Lipumba na Hamad wataachia ngazi kupisha uchaguzi mkuu
kufanyika.
Katika hafla maalumu ya kuagana na wajumbe wa Baraza Kuu
na watendaji wengine wa ngazi mbalimbali za chama hicho, Lipumba aliahidi kukubaliana na matokeo, iwapo atashindwa na
kwamba ataendelea kuunga mkono chama hicho kwa kutoa kila msaada unaostahiki.
“Nilikuwa mwanachama wa kawaida kwa kipindi kirefu ndipo
ikafika wakati chama kikaniteua kugombea na kuchaguliwa Mwenyekiti hadi leo,
kwa hivyo haki hii anaweza kuwa nayo mwanachama yeyote”, alisema Lipumba katika
hafla hiyo iliyofanyika nyumbani kwake.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa CUF, Hamad, alisema kila
mwanachama ana wajibu wa msingi wa kukijenga chama bila kujali wadhifa alionao.
Katika hafla hiyo iliyofanyika nyumbani kwa Profesa
Lipumba, Hamad alipongeza wajumbe wa Baraza kwa ushirikiano katika kipindi
chote cha miezi 64, hali ambayo alisema imeleta mafanikio makubwa ndani ya
chama.
Akizungumza namwandishi, Mkurugenzi wa Haki
za Binadamu, Habari na Uenezi wa chama hicho, Salim Biman, alisema Lipumba
anatetea nafasi ya uenyekiti, aliyoishika kwa zaidi ya miaka 10 sasa akipambana
na wenzake wawili. Alitaja wagombea
wengine wa nafasi hiyo ni Chifu Yemba
kutoka Shinyanga na M’bezi Adam Bakar kutoka Temeke, Dar es Salaam.
Katika nafasi ya Ukatibu Mkuu, Hamad ni mgombea pekee wa nafasi hiyo huku nafasi
ya Makamu Mwenyekiti wa chama hicho, ikiwaniwa na Juma Duni Haji ambaye pia ni mgombea pekee.
Makamu Mwenyekiti wa Chama hicho, Machano Khamis Ali,
amesema ameamua kwa hiari yake kutogombea tena, kutokana na sababu mbalimbali,
zikiwemo za kiafya
Aidha, alisema katika uchaguzi huo, pia kuna nafasi 45 za
ujumbe wa Baraza zinazowaniwa. Kati ya hizo,
20 ni wajumbe kutoka Zanzibar na 25 wajumbe kutoka Tanzania Bara na
uchaguzi wa Viti Maalumu.
“Kesho (leo) tunatarajia kuanza mkutano mkuu wa sita wa chama ambao kikatiba ndio mkubwa wenye
maamuzi makuu ya mwisho ya mambo mbalimbali ndani ya chama, ikiwemo kupitisha
wagombea wa nafasi mbalimbali katika uchaguzi wa ndani wa chama,” alisema
Bimani.
Alisema mkutano huo wenye wajumbe zaidi ya 800 kutoka
sehemu mbalimbali Bara na visiwani,
utafanyika kwa siku tano kuanzia leo
hadi Ijumaa, jijini Dar es Salaam.
No comments:
Post a Comment