Baraza la Ushauri la Watumiaji wa Huduma za
Maji na Nishati (EWURA CCC) limesema sekta za nishati na maji , zinakabiliwa na
changamoto ya watumiaji wa huduma hizo, kutokuwa na uelewa kuhusu haki na
wajibu wao, jambo linalotoa mwanya kwa watoa huduma kutowajibika.
Mwenyekiti wa Baraza la Ushauri la Watumiaji
wa Huduma za Maji na Nishati (EWURA CCC),
Profesa Jamidu Katima, alisema hayo juzi alipotembelea maadhimisho ya
Wiki ya Utumishi wa Umma, yanayohitimishwa leo kwenye Viwanja vya Mnazi Mmoja,
Dar es Salaam.
Profesa alitaka watoa huduma za nishati na
maji, kutumia maadhimisho hayo kuleta chachu ya kuboresha huduma, wanazozitoa
ili kuleta maendeleo katika sekta za maji na nishati.
Alisema
kiini cha kero nyingi zinazotolewa na watumiaji wa huduma za maji na
nishati, ni kukosekana kwa taarifa na elimu sahihi kutoka kwa watoa huduma na hivyo kusababisha maswali mengi
yasiyokuwa na majibu miongoni mwa watumiaji wa huduma za nishati na maji.
Alitaja baadhi ya kero zinazolalamikiwa na
watumia huduma za nishati na maji kuwa ni pamoja na ankara kubwa za umeme na maji , ambazo haziendani na
matumizi halisi ya wateja.
Alisema
mara nyingi malalamiko hutokana na ankara za kukadiria, upatikanaji
hafifu wa huduma za maji kwenye maeneo mengi ya miji, kukatizwa kwa huduma bila
kutoa taarifa, ucheleweshwaji wa kuunganishwa kwenye huduma husika baada ya
kukamilisha malipo stahiki na kauli zisizofaa kutoka kwa baadhi ya watumishi wa
taasisi husika.
Aidha, Profesa Katima alieleza kuwa, ingawa
mikataba ya huduma kwa wateja ni muhimu kama moja ya eneo linalotathmini
misingi ya utawala bora, mikataba hiyo haijawafikia watumiaji wengi wa huduma
za maji na nishati.
Baraza la Ushauri la Watumiaji wa Huduma zinazodhibitiwa
na EWURA lilianzishwa chini ya Kifungu namba 30 cha Sheria ya Mamlaka ya
Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji, Sura ya 414, lengo kuu likiwa ni kutetea
na kulinda maslahi ya watumiaji wa huduma za nishati na maji.
No comments:
Post a Comment