Polisi imetangaza operesheni nchi nzima ya kukamata
madereva wa pikipiki (bodaboda), wasiofuata sheria za usalama barabarani,
wakiwemo wanaopita taa nyekundu bila
kuruhusiwa.
Msemaji wa Jeshi la Polisi, Advera Senso alitoa
tamko jijini Dar es Salaam jana wakati akizungumza na waandishi
wa habari.
Licha ya operesheni kulenga kudhibiti madereva wa vyombo
hivyo wanaopita taa nyekundu, makosa mengine yatakayosababisha sheria kuchukua
mkondo wake ni kutozingatia alama na michoro ya usalama barabarani.
Operesheni hiyo itagusa waendesha pikipiki za kawaida, za
miguu mitatu(bajaj), baiskeli na maguta, ambazo kwa mujibu wa Polisi, zimekuwa
zikikiuka utaratibu na sheria za usalama barabarani.
“Jeshi la Polisi limekuwa likifanya juhudi za kuhakikisha
ajali za barabarani zinapungua, lakini bado kuna baadhi ya waendesha pikipiki,
baiskeli na maguta wamekuwa vinara wa kukiuka sheria, utaratibu na kanuni za
usalama barabarani.”
“Ukiukwaji huo unachangia ongezeko la ajali za mara kwa
mara ambazo zinaweza kuzuilika, hivyo tunaanzisha operesheni ya kubaini,
kukamata na kuwachukulia hatua kali za kisheria na kuwafikisha mahakamani.”
Kwa mujibu wa Senso, kuanzia Januari hadi Juni mwaka huu,
ajali 1,449 zilizosababishwa na bodaboda zilitokea na kusababisha vifo 218 na
majeruhi 1,304.
Alipoulizwa na waandishi wa habari juu ya kuwapo tabia ya baadhi ya polisi
kutumia operesheni kama hizo, kujiingizia kipato binafsi kwa kupokea rushwa,
Senso alisema, Polisi haijaanzisha operesheni hiyo kwa lengo hilo.
“Operesheni hii ni kwa ajili ya kuhakikisha madereva wanafuata
sheria za usalama barabarani,” alisisitiza Senso.
Ingawa
Senso alisisitiza operesheni hiyo kulenga madereva wanaokiuka sheria,
kumekuwepo na malalamiko dhidi ya baadhi ya askari, kugeuza madereva hao kama
mradi wa kujiingizia vipato binafsi.
Licha ya malalamiko kujitokeza kutoka maeneo
mbalimbali nchini, kwa upande wa Jiji la Dar es Salaam, baadhi ya askari
waliobatizwa jina la ‘Tigo’ pamoja na baadhi ya askari wa Kikosi cha Usalama
Barabarani, wanadaiwa kutoza faini za papo kwa hapo bila kutoa risiti.
Baadhi ya wakazi wa Dar es Salaam
walipendekeza Jeshi hilo la Polisi, hasa trafiki, waanze kuanzia sasa kutumia
Mashine za Kielektroniki za Malipo
(EFDs) za Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) katika kutoza faini za makosa
ya usalama barabarani.
Walisema utaratibu wa sasa wa trafiki,
kutumia lundo la vitabu barabarani,
linatia hofu kuwa fedha nyingi wanazotozwa madereva wa magari au
bodaboda kama faini, hazifikishwi serikalini, kwani kama zingefikishwa Serikali
ingekuwa na fedha nyingi.
Walisema mashine hizo za TRA, ndizo pekee
zitakazodhibiti fedha za Serikali na kuziba mianya yote ya ulaji wa trafiki.
Katika hatua nyingine, jeshi hilo la Polisi limetaka
vikundi vya ngoma kufuata taratibu kwa kuwa na vibali kutoka halmashauri za
maeneo husika ili kuzuia mianya ya ukiukaji maadili na kutoa mianya ya uhalifu.
“Polisi inakemea tabia iliyoibuka ya vikundi vya ngoma
maarufu kama vigodoro vinavyojihusisha na kupiga muziki au ngoma mitaani na
kufunga barabara kinyume na taratibu,” alisema.
No comments:
Post a Comment