SERIKALI YAFANYIA KAZI PENSHENI KWA WAZEE



Serikali imesema kuwa Mpango wa Pensheni kwa Wazee nchini, haujaanza kutekelezwa kutokana na kutokamilika kwa maandalizi.
Naibu Waziri wa Kazi na Ajira, Dk Makongoro Mahanga alisema hayo bungeni mjini hapa jana, alipojibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Leticia Nyerere (Chadema).
Dk Mahanga alisema kuwa hadi sasa kazi zifuatazo zimekamilika: Rasimu ya awali ya Mpango wa Pensheni kwa Wazee imeandaliwa; na ziara za mafunzo zimefanyika katika nchi za Kenya, Uganda, Mauritius, India, Thailand, Singapore, China na Indonesia.
Lengo la ziara hizo zilizohusisha pia wabunge, lilikuwa ni kujifunza na kupata uzoefu wa nchi nyingine katika kuendesha mipango ya pensheni kwa wazee.
Alisema maeneo ambayo maandalizi hayajakamilika ni pamoja na kubaini vyanzo endelevu vya mapato, vitakavyotumika kugharimia mpango huo, kuunda chombo kitakachosimamia pensheni, kupata maoni kuhusu mpango unaopendekezwa kutoka kwa wadau na taasisi zinazohusika; na kuwasilisha mpango huoƊ katika vyombo vya maamuzi.
Katika swali lake, Leticia alihoji "Tarehe 10 Oktoba 2010, Mheshimiwa Waziri Mkuu katika Siku ya Wazee Duniani aliahidi wazee kupewa mafao yao. Je, ni kwa nini mpango huo haujatekelezwa mpaka sasa?"
Akifafanua, Naibu Waziri alisema serikali inatambua umuhimu wa kuhakikisha watu wake wote, ikiwa ni pamoja na wazee, wanapata kinga ya hifadhi ya jamii.
Alisema katika kutekeleza azma hiyo , mwaka 2003 serikali ilipitisha Sera ya Taifa ya Hifadhi ya Jamii. Pamoja na mambo mengine sera hiyo, inaelekeza kuanzishwa kwa programu za misaada ya jamii, inayojumuisha pensheni ya jamii kwa wazee (universal pension).
Dk Mahanga alisema tamko la Waziri Mkuu la Oktoba Mosi 2010 wakati wa kuadhimisha Siku ya Wazee Duniani, lilitoa mwongozo wa kushughulikia suala la pensheni kwa wazee kwa kuagiza mamlaka zinazohusika, kuchukua hatua stahiki. Baada ya hapo, Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii (SSRA), ambayo ndiyo kwanza ilikuwa imeanzishwa, ilipewa jukumu la kushughulikia suala hilo.

No comments: