Utaratibu mpya wa kudhibiti msongamano wa
magari jijini Dar es Salaam, umetangazwa ambao utekelezaji wake utakapoanza,
pikipiki na bajaj hazitaruhusiwa kuegeshwa wala kuendeshwa katika njia za
waenda kwa miguu.
Utekelezaji huo unaotarajiwa kuanza hivi
karibuni, umelenga kuondoa msongamano, kuimarisha usalama na usafi katika
njia zote zilizokamilika za Mradi wa Mabasi yaendayo Haraka Dar es Salaam
(Dart).
Awamu ya kwanza ya mradi, inatekelezwa kutoka
Kimara hadi Kivukoni; Barabara ya Msimbazi kuanzia Faya hadi eneo la
Kariakoo-Gerezani na sehemu ya Barabara ya Kawawa kuanzia Magomeni hadi njia
panda ya Morocco.
Akizungumzia utaratibu huo mpya, Ofisa Mkuu
Mtendaji wa Wakala wa Mabasi yaendayo Haraka (DART), Asteria Mlambo
alisema magari yote, yatakayotumia mfumo wa njia hizo mpya, hayatatakiwa kuzidi
mwendo wa kilometa 50 kwa saa.
Alisema utaratibu huo, unaotarajiwa kuanza
hivi karibuni na kusimamiwa na mamlaka mbalimbali, ikiwemo Polisi Kikosi
cha Usalama Barabarani, mwendo huo usiozidi kilometa 50 utazingatiwa hasa
katika barabara ya Morogoro, ambayo mradi huo unakaribia kukamilika.
Chini ya utaratibu huo mpya, pia magari hasa
daladala, hayataruhusiwa kusimama njiani na pia itakuwa marufuku kufanya
biashara ndogo au biashara ya aina yoyote katika maeneo ya njia hizo.
“Kwa sasa tunaangalia maeneo ya muda ambayo
daladala zitaruhusiwa kusimama,” alisema Mlambo na kuongeza kuwa taratibu zote
zimekamilika na kwamba polisi wataanza kuhakikisha kuwa utaratibu huo,
unafuatwa hivi karibuni.
Vyombo vingine vitakavyosimamia utekelezaji wa
utaratibu huo licha ya Dart na Polisi, ni Mamlaka ya Usafiri wa Majini na Nchi
Kavu (Sumatra) na Wakala wa Barabara (Tanroads).
Kwa mujibu wa ofisa huyo wa Dart, kuegesha
magari au kufanya biashara katika maeneo ya waenda kwa miguu, hakutaruhusiwa na
watakaokiuka, watapewa adhabu kali.
“Napenda pia kuwataarifu wafanyabiashara
kuacha kupaki magari ya mizigo katika njia kuu na kupakua au kupakia mizigo,”
alisisitiza.
Wakati yapo mazoea ya madereva wa bajaji na
pikipiki, kuegesha vyombo vyao katika njia za watembea kwa miguu, Mlambo
alisema vyombo hivyo havitaruhusiwa tena kupita katika njia za waenda kwa
miguu.
“Makosa yatahusisha adhabu kali na faini ya
pesa taslimu,” alisema.
Alisisitiza utaratibu huo utakapoanza, kila
anayehusika hasa madereva katika jiji hilo kubwa la biashara, watatakiwa
kuuheshimu na kuufuata.
Mradi unaoendelea wa mabasi yaendayo haraka
katika Jiji la Dar es Salaam, unalenga kuimarisha huduma za usafiri na kuwa za
kisasa zaidi na kupunguza msongamano, ambao umekuwepo kwa kipindi kirefu sasa.
“Tunatarajia utaratibu huu kuanza hivi
karibuni,” Mlambo aliwaambia waandishi wa habari.
No comments:
Post a Comment